Partey akaribishwa rasmi Arsenal

London, England. Mchezaji mpya wa Arsenal, Thomas Partey ameonyesha jezi yake mpya ya klabu hiyo atakayaoitumia kwa mara ya kwanza, jambo ambalo limeonyesha nia ya ubingwa.

Kiungo huyo mkabaji alisajiliwa na Arsenal kwa ada ya uhamisho ya Pauni 45 milioni akitokea Atletico Madrid, usajili uliofanywa siku ya mwisho ya dirisha la usajili.

Nyota huyo wa kimataifa wa Ghana mwenye miaka 27, alionekana jana na fulana ya Gunners kwa mara ya kwanza tangu aliporipotiwa kusajiliwa kucheza katika Ligi Kuu England.

Partey, ambaye amepewa jezi yenye namba 18, atajiunga na wachezaji wanzake wa Arsenal baada ya kumaliza majukumu ya timu ya taifa ya Ghana.

Na mchezaji mwenzake mpya wa miamba hiyo, Runar Alex Runarsson alisema kusajiliwa kwa Partey kunaonyesha ishara kuwa klabu yao imedhamiria kufanya makubwa ndani na nje ya England.

Kipa huyo raia wa Iceland, ambaye amesajiliwa kutoka Dijon kwa uhamisho wa Pauni 1.6 milioni, alisema alifarijika kusikia kywa Partey amesajiliwa kabla ya kufungwa kwa usajili Oktoba 5.

Runarsson mwenye miaka 25 aliuambia mtandao wa Goal: “Nimefurahi sana kwasababu inaonyesha kuwa klabu imedhamiria makubwa, tunataka kurudi katika ubingwa wa Ligi Kuu England na Ligi ya Mabingwa Ulaya.

“Tunahitaji kuwamo na kufanya vizuri katika mashindano yote makubwa, na si kushiriki tu, tunahitaji kutwaa nmataji mengi iwezekanavyo.