Papa Shirandula afariki dunia

Muktasari:

Shemeji yake Ronald Wanyama amesema alipimwa na kukutwa na maambukizi ya virusi vya corona.

Nairobi, Kenya. Msanii maarufu wa vichekesho nchini Kenya Charles Bukeko (58) maarufu Papa Shirandula amefariki dunia leo Julai 18, 2020 asubuhi jijini Nairobi baada ya kuugua kwa muda mfupi.

Shemeji wa Bukeko, Ronald Wanyama amesema kabla ya umauti alipata wakati mgumu kwenye kupumua na kukimbizwa hospitali ya Karen.

“Ni huzuni hakuweza kutoka tena hospitali akiwa mzima. Alipimwa na kukutwa na corona. Tumechanganyikiwa” amesema Wanyama

Wanyama amesema Papa Shirandula alisafiri kwenda Western na kurudi Nairobi Jumapili kabla ya kuanza kuumwa.

Enzi za uhai wake Shirandula alikuwa muigizaji mkuu wa tamthilia ya vichekesho inayofahamika kwa jina la Papa Shirandula ikionyeshwa Citizen TV. Ameshinda tuzo mbalimbali ikiwemo za Kalasha katika kipengele cha muigizaji bora wa tamthilia za luninga mwaka 2010.

Shirandula ameacha mke na watoto watatu.