Onyango, Wawa wamtia kiburi Gomes

ANGALIA msimamo wa Ligi Kuu Bara na matokeo ya mechi za awali na zile za makundi za Ligi ya Mabingwa Afrika ilizocheza Simba uone namna gani ukuta wa timu huyo ulivyo mgumu na jambo hilo limempa kiburi Kocha Gomes wakijiandaa kuvaana na Yanga Jumamosi.

Simba imeruhusu mabao 10 tu hadi sasa katika Ligi Kuu kupitia mechi zao 25, huku kwenye mechi za kimataifa imefungwa matatu tu katika mechi zao 10 na katika Kombe la ASFC imefungwa moja tu la juzi dhidi ya Kagera Sugar na hilo limemfanya Gomes kuchekelea.

Akizungumza kuelekea pambano lao na Yanga, kocha huyo kutoka Ufaransa alisema anafurahi anaenda kukutana na watani wao, akiwa na ukuta usioruhusu mabao kirahisi.

“Taswira nzuri kuwa tunaenda kucheza mechi ya dabi huku mabeki wangu wakiwa wameruhusu mabao machache na halitakuwa jambo la kushangaza kuona waliendeleza hilo katika mchezo huo,” alisema Gomes ambaye ukuta wake unaundwa na kipa Aishi Manula, Shomary Kapombe, Mohammed Hussein, Pascal Wawa, Joash Onyango na Taddeo Lwanga anaowatumia kikosi chake cha kwanza, huku kina Benno Kakolanya, David Kameta, Gadiel Michael, Kennedy Juma, Ibrahim Ame na Jonas Mkude wakitumika katika baadhi ya timu au kuanzia benchi kama wachezaji wa akiba.

Gomes pia ana safu hatari ya ushambuliaji.