Olunga kujiunga na Al-Duhail ya Qatar

Tokyo, Japan. Taarifa za kuaminika kutoka nchini Japan, zinasema kuwa Straika wa Harambee Stars, Michael Olunga anayechezea Kashiwa Reysol, inayoshiriki ligi kuu ya Japan, J1 League, yuko mbioni kujiunga na klabu ya Al-Duhail ya Qatar.

Kwa wiki moja sasa kumekuwa na tetesi za mshambuliaji huyo, aliyetwaa tuzo ya mchezaji bora wa msimu, pamoja na ile ya mfungaji bora, baada ya kupachika mabao 28 wavuni, kwenye mechi 32 alizocheza, yuko mbioni kugura klabu hiyo.

Kwa mujibu wa vyanzo mbalimbali vya Habari nchini Japan, ni kwamba klabu hiyo hatimaye imekubali kumuuza straika huyo wa zamani wa Thika United, Tusker FC na Gor Mahia, kwa dau la euro 7 milioni, sawa na Ksh940 milioni au Tsh 19 bilioni.

Aidha, Al-Duhail pia inadaiwa kumhakikishia Olunga, mwenye umri wa miaka 26, kitita kizuri cha mshahara endapo  atajiunga nao na sasa, kuna uhakika wa asilimia 89 kuwa, injinia atacheza kwenye ligi kuu ya Qatar msimu ujao.

Msukumo wa kumpata straika mzuri, atakayeongoza mashambulizi ya klabu hii, imekuja baada ya Nyota wa zamani wa Juventus Mario Mandzukic kugura, miezi sita tu baada ya kujiunga nao, Julai mwaka jana.


Imeandikwa na Fadhili Athuman