Olunga afukuzia 1m za kiatu

Olunga afukuzia Ksh1 millioni za kiatu

NAHODHA wa Harambee Stars Michael ‘Engineer’ Olunga anazidi kukifukizia kiatu cha dhahabu kwenye ligi kuu ya Qatar Stars League (QNB).

Mpaka sasa Olunga ndiye top scorer kwenye ligi hiyo akiwa na mabao 19.

Wikendi ya Jumamosi, Engineer alipachika mabao mawili kwenye ushindi wa mabao 4-0 timu yake Al Duhail ilipochuana na Al Rayyan.

Mpinzani wake wa karibu ni straika wing’a na nahodha wa Ghana Andre Ayew anayeichezea Al Sadd akiwa ametinga mabao 12.

Al Sadd wanaongoza msimamo wajedwali wakiwa na alama 43, baada ya mechi 15. Kikosi cha Olunga ambao ndio mabingwa watetezi kinakamata nafasi ya pili kwa pointi 36. Hata hivyo Al Duhail wamecheza mechi mbili zaidi ya vinara Al Sadd.

Olunga alijiunga na Al Duhail msimu huu na alitawazwa mchezaji bora wa Oktoba/Novemba baada ya kupachika mabao matano kwenye mechi tano alizocheza katika kipindi hicho.

Endapo atafanikiwa kumaliza kama mfungaji bora msimu huu wa 2021/22, atatuzwa kiasi kisichopungua dola 10,000.