Nusu fainali ya kibabe Afcon U-20

PATACHIMBIKA! ndivyo unaweza kusema kuelekea kesho Jumatatu kwenye michezo ya nusu fainali ya michuano ya mataifa ya Afrika kwa vijana chini ya miaka 20 (Afcon U-20) nchini Mauritania.

Timu za Uganda, Ghana, Gambia na Tunisia ndizo zilitinga hatua hiyo na mchezo wa kwanza utapigwa saa 10:00 kati ya Ghana ambaye ni mabingwa mara tatu wa taji hilo watakuwa na shughuli pevu mbele ya Gambia ambao waliwahi kuwa washindi wa tatu wa michuano hiyo mwaka 2007.

Mchezo mwingine utapigwa kati ya Uganda ambao ndio mara yao ya kwanza kufika hatua hiyo wao watavaana na Tunisia saa 1:30 usiku.

Mechi zote hizo zinatarajiwa kupigwa Uwnaja wa Stade Olympique katika Jiji la Nouakchott.

Washindi wa mechi hizo watakuwa wameingia hatua ya fainali itakayochukua nafasi kwenye dimba la Stade Cheikha Ould Boidiya, Machi 6.

Wakati wale ambao watapoteza watatajitupa kwenye mechi ya kuwania mshindi wa tatu itakayochezwa Uwanja wa Stade Olympique, Machi 5. 

Ikumbukwe timu ya taifa ya Tanzania 'Ngorongoro Heroes' ilishiriki michuano hiyo na kutolewa hatua ya makundi.