Njia ya Jangwani yafungwa, Simba ikijiandaa kuwakera watani wao
Muktasari:
- Kwa mujibu wa ratiba ya awali, msafara wa Simba ulipaswa kupita Jangwani kabla ya kuelekea Msimbazi na baadaye kuhitimisha shamrashamra zake katika fukwe za Coco.
WAKATI msafara wa Simba wa kusherehekea ubingwa wa Kombe la Shirikisho la CRDB ukiendelea katika mitaa mbalimbali ya Dar es Salaam, bado haijajulikana utakavyopita eneo la Jangwani baada ya njia hiyo kufungwa.
Kwa mujibu wa ratiba ya awali, msafara wa Simba ulipaswa kupita Jangwani kabla ya kuelekea Msimbazi na baadaye kuhitimisha shamrashamra zake katika fukwe za Coco.
Hata hivyo, taarifa kutoka eneo hilo zinabainisha kuwa barabara ya Jangwani imefungwa kufuatia shughuli za Yanga, ambayo jana, Jumamosi, ilifanya paredi ya kusherehekea ubingwa wa Ligi Kuu ya NBC.
Katika paredi hiyo, Yanga ilianzia Karume, ikapita Msimbazi kabla ya kuhitimisha msafara wao Jangwani.
Kutokana na hali hiyo, bado kuna sintofahamu kuhusu namna msafara wa Simba utakavyopita pindi utakapofika eneo la Jangwani huku mashabiki wakisubiri kuona kama utaruhusiwa kuendelea kama ilivyopangwa au waandaaji na vyombo vya usalama wataelekeza kutumia njia mbadala.
Mpaka sasa, hakuna taarifa rasmi iliyotolewa kuhusu mabadiliko yoyote ya ratiba ya msafara huo huku wengi wakisubiri kuona nini kitatokea mara baada ya msafara wa Simba utakapowasili hapo.