Mwambusi apewa mikoba Yanga

KOCHA Juma Mwambusi ndiye atashika usukani wa kuinoa Yanga, wakati mchakato wa kusaka mbadala wa Cedrick  Kaze aliyeachishwa kazi baada ya kutoka sare ya bao 1-1 na Polisi Tanzania, unaendelea.

Mwambusi ametangazwa rasmi na mwenyekiti wa klabu hiyo, Mshindo Msolla kwamba Mwambusi atashika nafasi hiyo, wakati wanaendelea kusubilia CV za makocha ambao wanahitaji kazi.

"Bahati mzuri Mwambusi aliondoka vizuri, kwani alikuwa anaumwa ndio maana aliomba apumzike na Yanga ilimsaidia matibabu na Mungu amesaidia anaendelea vizuri,  hana ugeni na timu, kwani alianza nayo msimu huu na alikuwepo Kombe la Mapinduzi," amesema na ameongeza kuwa;

"CV za makocha ambao wataomba kazi zitapelekwa kamati ya ufundi ambako kuna wachezaji na makocha, hivyo tunaamini kila kitu kitakwenda sawa, ila kwasasa Mwambusi ndiye ataendelea na majukumu hayo," amesema Msolla.

Kaze ameachishwa kazi baada ya kukiongoza kikosi hicho katika mechi 18, kilishinda michezo 10, sare saba na kilipoteza mmoja dhidi ya Coastal Union ya Tanga kwa mabao 2-1.