Muguna aaga Gor, huyoo njiani kutua Azam

Muktasari:

Keneth Muguna wakati wowote atatambulishwa kuwa nyota mpya wa Azam FC ambayo imeshinda vita ya kuwania saini ya kiungo huyo raia wa Kenya.


Kiungo wa Gor Mahia ya Kenya Kenneth Muguna rasmi amewaaga mashabiki, viongozi na wachezaji wenzake huku akizidisha uwezekano wa kutua Azam FC.

Akitumia ukurasa wake wa Instagram Muguna ameandika kwamba wakati umefika kwake kuanza kuangalia changamoto mpya katika maisya yake ya soka.

Hata hivyo Muguna ameishukuru Gor Mahia kwa nafasi ambayo walimpa kuitumikia akifika hapo akiwa kijana mdogo lakini akapata nafasi ya kuonyesha kipaji chake.

Aliongeza kwamba:"Sikutarajia kama mambo yangekwenda kirahisi ukizingatia nilikuta wachezaji bora wenye uwezo mkubwa lakini bado (mashabiki na viongozi) mlinifanya mambo niyaone rahisi,"aliandika Muguna

"Angalia niliyofanikiwa hapa klabuni,nimeridhika,nimekuwa nabahati kubwa kuwa chini ya makocha wakubwa na uongozi imara,nakushukuru mwenyekiti a uongozi kwa ujumla kwa ushirikiano wa kuongeza mkataba ingawa hatukuweza kuukamilisha sasa nahitaji changamoto mpya.

"Nawashukuru kwa miaka yote tuliyokuwa pamoja na naamini mtafurahia katika mechi zilizosalia,"aliandika Muguna.

Wakati Muguna akiaga habari za uhakika ni kwamba Azam FC ilishamalizana naye na wakati wowote watamtambulisha wiki hii kuwa kiungo wao mpya.

Tayari Azam FC imeshawatambulisha nyota wanne ambao ni Wazambia watatu kiungo Paul Katema,winga Charles Zulu,mshambuliaji Rodgers Kola na beki mzawa Edward Manyama.