Mtenje atimkia Fountain Gate

Muktasari:
- Katibu Mkuu wa Dodoma Jiji, Fortunatus Johnson alikiri kufikia makubaliano ya pande mbili ya kusitisha mkataba na nyota huyo, huku akiweka wazi asingependa kueleza zaidi sababu zilizosababisha maamuzi hayo kufikiwa kutokana na kuheshimiana.
Dodoma Jiji imefikia makubaliano ya kuvunja mkataba na aliyekuwa kiungo mkabaji wa kikosi hicho, Mtenje Albano, huku taarifa zikieleza nyota huyo yuko katika hatua za mwisho za kujiunga na Fountain Gate ya mkoani Babati Manyara.
Katibu Mkuu wa Dodoma Jiji, Fortunatus Johnson alikiri kufikia makubaliano ya pande mbili ya kusitisha mkataba na nyota huyo, huku akiweka wazi asingependa kueleza zaidi sababu zilizosababisha maamuzi hayo kufikiwa kutokana na kuheshimiana.
“Nikiri wazi kweli tumefikia makubaliano ya kuvunja mkataba na Mtenje na kama utakumbuka tuliingia naye makubaliano ya miaka miwili na ameshatumikia mmoja na nusu, narudia uamuzi huo ni wa pande zote mbili hivyo tuheshimu kilichotokea.”
Wakati maamuzi hayo yakifanyika, taarifa ambazo Mwanaspoti imezipata zinaeleza mabosi wa Fountain Gate wamewasiliana juu ya kupata saini ya nyota huyo, huku mazungumzo yakiwa pia katika hatua nzuri kwa ajili ya kuongeza nguvu kikosini humo.
“Albano ni kiungo mzuri na ni pendekezo la kocha wetu, Mohamed Muya kwa sababu katika mapendekezo yake aligusia pia eneo hilo, naamini ataongeza ushindani kwani hakuna mtu yeyote asiyejua uwezo wake kwenye timu alizochezea,” kilisema chanzo chetu.
Usajili wa nyota huyo unamfanya kwenda kuungana na mastaa wengine wapya waliosajiliwa dirisha hili dogo ambao ni Faria Ondongo na Said Mbatty kutoka Tabora United, Jimmyson Mwanuke (Singida Black Stars) na Jackson Shiga aliyetokea Coastal Union.