Mtanzania aibuka wa kwanza mashindano ya dunia kuogelea

Muktasari:

Mhini alionyesha uwezo mkubwa na kuibuka katika nafasi ya kwanza katika mtindo wa Backstroke kwa kutumia muda wa 1.04,27 na kuwashinda waogeleaji wengine

Dar es Salaam. Nahodha wa timu ya Taifa ya kuogelea, Dennis Mhini ameng’ara katika hatua ya mchujo ya mashindano ya Dunia yanayoendelea mjini Budapest, Hungary baada ya kuongoza katika kundi la kwanza mchujo.

Mhini alionyesha uwezo mkubwa na kuibuka katika nafasi ya kwanza katika mtindo wa Backstroke kwa kutumia muda wa 1.04,27 na kuwashinda waogeleaji wengine.

Muogeleaji huyo anayesoma shule ya St Felix ya Uingereza, alianza kuongoza tangu kengere ya kuanzisha mashindano hayo na kuwapita wenzake kwa mbali.

Waogeleaj ambao alishindana nao ni Ared Ruci (Albania), Mandresy Rajaonson (Madagascar), Adewole Adekoya (Nigeria). Pia walikuwemo Humza Khaliq wa Pakistan, Tsitocina Razanatefy (Madagascar), Amar Altub Ali Altub wa Sudani na Mtanzania mwingine, Isam Sepetu.

"Nimefuraji kushika nafasi ya kwanza kwenye kundi langu na hii inaonyesha jinsi gani mchezo wa kuogelea unashika kasi pamoja na kuwepo kwa changamoto mbalimbali has kukosa bwawa la kuogelea la kisasa la mchezo huo," alisema Mhini.

Alisema kuwa waogeleaji wa Tanzania wamekuwa na kilio cha kupata bwawa la mita 50 la kisasa kwa kipindi kirefu na kushindwa kuzoea vifaa vya kisasa.

Mabwawa mengi ambayo yanamilikiwa na taasisi binafsi (zaidi shule za kimataifa) yana urefu wa mita 25 na kukosa vifaa vya kisasa kama ‘diving block’ (kifaa kinachutumiwa na waogeaji kuchupa) na touchpad ambayo inatumika kwa ajili ya kurekodi muda.