Msikie Msuva auota ubingwa Afrika 

NYOTA wa Wydad Casablanca, Simon Msuva ameweka wazi dhamira yake ya kutamani kutwaa ubingwa wa Ligi ya Mabingwa Afrika baada ya kutinga hatua ya makundi huku ndugu zao Raja Casablanca wakiangukia pua kwenye kinyang’anyiro hicho. 
Wydad Casablanca ambao walitandikwa bao 1-0 kwenye mchezo wa kwanza, walipindua meza kibabe wakiwa nyumbani baada ya kutoa dozi ya mabao 3-0 kwa Stade Malien Bamako na kutinga hatua ya makundi kwa ushindi wa jumla ya mabao 3-1. 
Ndugu zao, Raja Casablanca wamejikuta wakigonga mwamba mbele ya Teungueth FC ya Senegal baada ya kutupwa nje kwa mikwaju ya penati 3-1 baada ya kutoka suluhu (0-0) kwenye michezo yote miwili, nyumbani na ugenini. 


Msuva anaamini wananafasi ya kutwaa ubingwa wa Afrika japo sio kazi nyepesi na ili kuthibitika hilo kwenye uhalisia wanatakiwa kuonyesha ubora wao kwenye makundi. 
“Unapokuwa timu kubwa mawazo na mipango huwa tofauti, nilivyocheza kwa mara ya kwanza Ligi ya Mabingwa nikiwa na Difaa, haikuwa lengo kutwaa ubingwa na kama tungetwaa yangekuwa maajabu kwa sababu nguvu yetu ya ushindani haikuwa kubwa tukilinganisha na wapinzani wetu,” 
“Naona kwa ukubwa wa kikosi chetu tunauwezo wa kukabiliana na timu yoyote na tukatoboa, kwangu nafasi ya kuonyesha kuwa tunautaka ubingwa ni kuanza kwa kuonyesha makali yetu kwenye hatua ya makundi, najua inawezekana,” alisema na kuongeza. 
Katika mchezo ambao Wydad Casablanca iliwashikisha adabu Teungueth FC kwa mabao 3-0, Msuva alitoa asisti ya miongoni mwa mabao aliyofunga Muaid Ellafi aliyepiga mabao matatu ‘hat trick’ na kuondoka na mpira wake kwapani. Chama la Msuva limepangwa kundi C kwenye Ligi ya Mabingwa Afrika likiwa na Horoya anayoichezea mshambuliaji wa zamani wa Yanga, Heritier Makambo, Petro de Luanda ya Angola na Kaizer Chiefs ya Afrika Kusini.