Mogella: Dirisha la usajili kipimo cha thamani za wachezaji

Muktasari:

Imeelezwa kwamba kipindi cha usajili kitakuwa cha manufaa kwa wachezaji walikuwa na viwango vya juu msimu huu, hasara kwa wale huduma zao zilikuwa hafifu.

Dar es Salaam. Nyota wa zamani wa Simba, Zamoyoni Mogella amesema hakuna kipindi kizuri kwa wachezaji kama cha usajili kinaonyesha thamani ya kile walichokifanya kwa msimu mzima.

Mogella alisema ili mchezaji ajue thamani yake ni pale mkataba wake unapomalizika atajipima kwa dau atakalopewa na waajiri wake.

Mogella alisema mchezaji aliyefanya vizuri na kuibeba klabu alioitumika wakati wa usajili kwake ni kicheko.

"Wakati wa usajili kuna mambo mawili kwa maana ya wale ambao viwango vyao vilikuwa tishio lazima watavuna mamilioni ya pesa kwa maana kila klabu itataka kuwatumia.

"Lakini kwa wale ambao huduma yao haikuwa ya muhimu na hawakupata muda wa kucheza basi watakuwa na changamoto ya kusajiliwa kwa hasara.

"Hili ni funzo kwa wachezaji kuwa wawajibikaji kwa asilimia mia pindi wanapopewa nafasi na makocha wao ili mwisho wa siku waweze kuvuna matunda ya vipaji vyao," alisema Mogella.