MO Dewji amlilia Manji
Muktasari:
- Manji alifariki Jumamosi iliyopita na kuzikwa Jumatatu nchini Marekani.
Dar es Salaam. Mwekezaji wa Simba, Mohammed Dewji ametuma salamu za rambirambi kwa familia ya aliyewahi kuwa mwenyekiti na mfadhili wa Yanga, Yusuf Manji aliyefariki Jumamosi iliyopita huko Marekani ambako pia alizikwa jana akisema kifo hicho kimemuacha na majonzi.
Katika taarifa yake aliyoitoa leo, Dewji alisema kuwa pamoja na utofauti wa itikadi za kishabiki kwa timu za Simba na Yanga ambazo walikuwa nazo tangu utotoni, walikuwa marafiki wakubwa na kifo hicho kimemgusa.
“Kwa masikitiko makubwa nimepokea taarifa za kufariki kwa Yusuf Manji, rafiki wa rika langu kwa siku nyingi. Yusuf na mimi tulikutana kwa mara ya kwanza tukiwa na umri wa miaka 12 tu. Kuanzia darasani ambapo tulishiriki masomo mengi na kufanya kazi kwenye miradi pamoja, hadi mijadala yetu ya kusisimua kuhusu soka - kujitolea kwangu kwa Simba na mapenzi yake kwa Yanga.
“Uhusiano wetu ulikuwa imara. Safari ya Yusuf ilimchukua kutoka New York hadi Atalanta, huku barabara yangu ikielekea D.C. (Washington)kufuata elimu yangu. Dhamira ya Yusuf kwa Yanga ilikuwa kubwa; hakuwekeza rasilimali zake tu, bali alisema roho yake ndani ya timu hiyo, na kuiletea mafanikio makubwa na kutengeneza historia ambayo Yanga itaikumbuka milele,” alisema Dewji.
Dewji alisema kuwa kifo cha Manji ni pigo kubwa kwake, ndugu, jamaa na marafiki.
“Leo, ninaomboleza mtu ambaye alikuwa mshindani mkali, rafiki, na roho ya ukarimu. Yusuf alitumia kwa wingi vitu alivyokuwa akiviamini, na athari yake kwa wale waliokuwa karibu naye ilikuwa kweli isiyopimika.
“Tunapoomba kwa ajili ya nafsi yake kupata amani ya milele, pia tunatuma rambirambi zetu za kina kwa familia yake, mama yake, dada yake, mke na watoto. Aliwapenda sana, na najua walihisi upendo huo kila siku.
“Yusuf, kuondoka kwako kunaacha pengo mioyoni mwetu, lakini tunafarijiwa na kumbukumbu na athari kubwa ulizoziacha. Tunaposema kwa Kiswahili, “Nyinyi, mmetangulia na sisi tupo nyuma yenu.
“Umeenda mbele, na sisi tuko nyuma yako. Pumzika kwa amani rafiki yangu. Tutakukosa milele lakini hautasahaulika,” alisema Dewji.