Mlandege yajiweka pazuri mbio ubingwa ZPL

Muktasari:
- Timu tano zilizopo katika mbio za ubingwa wa Ligi Kuu Zanzibar msimu huu ni: watetezi JKU, KVZ, Mafunzo, Mlandege na Mwembe Makumbi, huku nne zinazopambana kuepuka kuungana na Tekeleza na Inter Zanzibar katika kushuka daraja ni; Chipukizi, Junguni United, Mwenge na Kipanga.
MABINGWA wa Kombe la Mapinduzi, Mlandege imeendelea kuufukuzia ubingwa wa Ligi Kuu Zanzibar (ZPL), baada ya kuichapa Mwenge kwa bao 1-0 katika mechi iliyopigwa jana kwenye Uwanja wa Mao A, mjini Unguja.
Bao hilo pekee lililoipa Mlandege poinri tatu muhimu lilifungwa na Mussa Hassan dakika ya 63.
Licha ya Mlandege kutoka na ushindi, lakini ilionekana haina muunganiko na wachezaji walikuwa wanapoteana wakati wakutengeneza nafasi za mashambulizi katika lango la Mwenge.
Matokeo hayo yameifanya Mlandege ambao ni mabingwa wa Kombe la Mapinduzi kwa msimu wa pili mfululizo imefikisha pointi 50 kupitia mechi 26.
Katika mechi nyingine, Watetezi wa Ligi hiyo, JKU ilitakata kwa kupata ushindi wa bao 1-0 dhidi ya Chipukizi kwenye Uwanja wa FFU Finya uliopo visiwani Pemba.
Yakoub Amour ndiye aliyefunga bao hilo dakika ya sita tu ya mchezo na kudumu hadi dakika 90.