Mbabe, Kiduku kimeeleweka

Muktasari:

  • Kiduku mwenye pointi 3.030 atapanda ulingoni akiwa bondia namba moja nchini kwenye uzani wa super middle na Mbabe mwenye pointi 1.351 akiwa namba mbili kati ya mabondia 14 kwenye uzani huo, wote wana nyota mbili.

Pambano la marudiano kati ya mabondia wenye upinzani, Twaha 'Kiduku' Kassim na Abdallah Pazi 'Dullah Mbabe' sasa litapigwa Julai 24, 2021 jijini Dar es Salaam.

Tayari mabondia hao wamesaini mkataba kuzichapa pambano hilo ambalo litakuwa la tatu kuwakutanisha.

Awali walizichapa na kutoka sare, matokeo ambayo yaliibua sintofahamu kila upande ukiyapinga kabla ya kucheza tena Agosti 28, 2020 kwenye uwanja wa Uhuru, Dar es Salaam na Mbabe kuchapwa kwa ponti katika uzani wa super middle.

Refarii, Emmanuel Mlundwa alimtangaza Kiduku kuwa mshindi baada ya kuongoza raundi zote 10 na majaji wote kumpa ushindi.

Majaji, Chaurembo Palasa na Anthony Ruta walitoa pointi 97-93 kila mmoja na Modest Rashid alitoa pointi 99-91 kwa Kiduku, matokeo ambayo Mbabe aliyakubali na kuomba pambano jingine la marudiano.

Kiduku bondia wa 83 duniani atapanda ulingoni akibebwa na rekodi wakati Mbabe bondia wa 128 kati ya 1199 akibebwa na uzoefu.

Mbabe mpaka sasa amepigana mapambano 39, ameshinda mapambano 29 (26 KO), amepigwa mara 9 (2 KO) na kutoka sare pambano moja.

Wakati Kiduku ameshapigana mapambano 25, ameshinda mapambano 17 (8 kwa kO). amepigwa mara 7 (1 kwa KO) na kutoka sare pambano moja, wote wanatumia zaidi mkono wa kushoto (orthodox).