Man City yapewa wiki kwa Koulibaly

MANCHESTER, ENGLAND. MANCHESTER City imeripotiwa kupewa wiki hii tu kuhakikisha inakamilisha dili la beki wa kati Kalidou Koulibaly hadi itakapofika wikiendi kila kitu kiwe kimeeleweka.

Gazzetta dello Sport linaripoti Napoli wamechoshwa na ngojangoja ya Man City, hivyo wanataka wakamilishe dili kama kweli wanamtaka beki huyo wa kati ili wao watazame namna ya kuziba pengo lake.

Napoli inamuuza beki huyo kwa Pauni 70 milioni, lakini Man City bado wanasuasua kulipa mkwanja huo.

Kocha wa Man City, Pep Guardiola anahitaji huduma ya Koulibaly kwenye kikosi chake licha ya kwamba amekuwa akimfukuzia pia beki wa Atletico Madrid, Jose Gimenez.

Napoli wamegoma kumuuza kwa bei ndogo ambapo kocha wao Gennaro Gattuso alisema Jumapili iliyopita, Koulibaly hawezi kuuzwa kwa bei chee.