Kiungo Simba aituliza Ruvu

KIUNGO wa Simba, Abdulsamad Kassim ametuliza presha katika kikosi cha Ruvu Shooting baada ya kujiunga nao kwa mkopo katika dirisha dogo la usajili litakalofungwa kesho Jumamosi hii.

Kujiunga kwake ndani ya Ruvu pia kumemfanya kupumua Kocha Mkuu wa chama hilo, Boniphace Mkwasa ambaye hapo awali alihaha kupata wachezaji bora bora baada ya nyota wake zaidi ya 10 kwenda kwenye kozi ya ajira ya Jeshi.

Mkwasa amemuelezea Abdulsamad ataongeza kitu ndani ya timu yake na kufanya iendelee kupambana kuhakikisha inatimiza malengo iliyojiwekea kwa msimu huu.

“Ni mchezaji mzuri, naamini kwa kushirikiana na wenzake timu itakuwa imara zaidi, hapo mwazo nilikuwa na wasiwasi wa XXkupata wachezaji bora baada ya waliokuwepo kuondoka lakini ujio wa Abdulsamad na wenzake umenipa imani kuelekea mechi zijazo,” alisema Mkwasa.

Naye Abdulsamad alifunguka kuwa anaenda Ruvu kufanya kazi na kuonesha kiwango bora ambacho Simba hakupata nafasi ya kucheza.

“Nadhani Ruvu nitapata nafasi ya kucheza, naenda kuonesha ubora wangu kule maana ni timu nzuri hivyo nitahakikisha naipambania ili ifikie malengo yake na mimi nizidi kuboresha na kuonesha uwezo wangu,” alisema Abdulsamad.