Kapombe, Manula na Chama wachuana mchezaji bora Aprili

Muktasari:

Katika kuwapa motisha na morali zaidi klabu ya Simba ilianzisha tuzo ya mchezaji mpya wa mwezi ambapo mpaka sasa imetwaliwa na Luis na Onyango

MASTAA watatu wa Wekundu wa Msimbazi Simba, wameingia katika kinyang'anyiro cha kumsaka aliyeng'ara zaidi mwezi uliopita.

Walioingia katika kinyang'anyiro hicho ni Clatous Chama Raia wa Zambia, Aishi Manula na Shomari Kapombe ambao mmoja wao ataibuka mshindi.

Mshindi anapatikana kupitia idadi kubwa ya kura atakazopata kupitia kwa wanasimba kupitia tovuti ya klabu ya Simba.

Kwa mujibu wa Simba nyota watano waliingia kwenye kinyang’anyiro hicho lakini Kamati maalumu iliwachuja na kubaki na watatu ambao watapigiwa kura na mashabiki.

Nyota wawili ambao walifika hatua hiyo ya tano bora ni Luis Miquissone na Pascal Wawa.

Tuzo hii ambayo inadhaminiwa na Emirate Aluminium Profile itakuwa ni ya tatu kutolewa tangu ilipoanza mwezi Februari mwaka huu.

Mchezaji atakayepata kura nyingi atakabidhiwa tuzo na fedha taslimu Sh 1,000,000 kutoka kwa wadhamini hao.

Miquissone alikuwa mchezaji wa kwanza kutwaa tuzo hiyoFebruari wakati Joash Onyango alishinda mwezi Machi.