Kagere ndio kwaanzaa!

KINARA wa mabao kwenye kikosi cha Simba, Meddie Kagere amesema kushindwa kupata nafasi ya kucheza kikosi hicho katika nyakati tofauti ilikuwa kama changamoto zilizomfanya kuongeza juhudi zaidi.

Alisema pengine mabadiliko ya kocha yanaweza kumrudisha kwenye kasi yake kwani kila mmoja huwa na machaguo yake lakini hata akipata dakika chache za kucheza anapenda kufanya jambo la kuisaidia timu ili kuonekana yupo.

“Nikipata hata muda mchache wa kucheza napenda kujituma na kuisaidia timu kwa kufunga mabao kama nitapata nafasi ya kufanya hivyo au kumsaidia mwingine kufunga kulingana na majukumu ya nafasi yangu yalivyo,” alisema Kagere mwenye mabao manne katika Ligi Kuu Bara mpaka sasa.

Mnyarwanda huyo alisema malengo yake katika kikosi cha Simba msimu huu ni kuhakikisha anapata nafasi ya kucheza mara kwa mara na ili aweze kuisaidia timu.

Kagere alisema akiwa anapata nafasi hiyo jukumu la kwanza katika nafasi yake ni kufunga mabao kadri ambavyo atapata nafasi ya kufanya hivyo ili kutimiza lengo la timu kushinda kila mchezo.

Alisema baada ya hapo mambo mengine kama ya kufunga mabao mengi yanakuja kwa sasa hivi anahitaji kuweka kambani mabao 13, kama ambavyo alifanya msimu uliopita kwenye ligi.

“Ligi ndio kwanza ipo mzunguko wa sita na ushindani ni mkubwa mno katika kila timu kwahiyo ni mapema kuzungumza mambo mengi zaidi tusubiri kwanza michezo ijayo,”aliongeza.

Kagere msimu huu ameifungia Simba mabao manne kwenye mechi dhidi ya Dodoma Jiji, Namungo, mawili dhidi ya Ruvu Shooting na yote yalikuwa muhimu kwani yaliipa timu hiyo ushindi.