Joshua akomaa Yanga

Beki wa Yanga, Oscar Joshua
Muktasari:
Akizungumza na Mwanaspoti hivi karibuni Joshua alisema “Asilimia kubwa ya maendeleo yangu yametokana na Yanga, najua hiki ni kipindi cha mpito napambana nitarejea kwenye kikosi cha kwanza,” alisema.
BEKI wa Yanga, Oscar Joshua ameonekana kukosa namba ndani ya kikosi hicho, ila yeye amefichua kwamba pamoja na changamoto hiyo ana siri nzito na Yanga.
Akizungumza na Mwanaspoti hivi karibuni Joshua alisema “Asilimia kubwa ya maendeleo yangu yametokana na Yanga, najua hiki ni kipindi cha mpito napambana nitarejea kwenye kikosi cha kwanza,” alisema.
Akijibu swali kama ana mpango wa kuachana na timu hiyo! Joshua alijieleza kuwa: “Siwezi kusema nitafia Yanga ingawa siwezi kusema naondoka Yanga kwa sasa ila kila kitu kina wakati wake ,”
Aliongeza kuwa: “Ikifika wakati wa kuondoka nitaondoka hata kama ningependa kubaki kwani kila kazi ina changamoto zake kikubwa ni namna ya kuzikabili,” alisema.
Joshua alisema sababu iliyompelekea kutoonekana uwanjani kwa muda ni kusumbuliwa kwa majeruhi lakini kwa sasa yupo fiti.
“Naendelea na mazoezi ya timu na yangu binafsi, naamini nitacheza kwani hakuna anayeweza kujimilikisha namba, kocha anaangalia mchezaji ambaye anakuwa msaada ndani ya timu,” alisema.