Huyu Wenger anawashangaa Pogba, Sancho

PARIS. UFARANSA. ARSENE Wenger anashangaa kuona Jadon Sancho na Paul Pogba wanasumbua muda mrefu kwenye usajili duniani.

Pogba kwa sasa yupo Manchester United, lakini jina lake kwa muda mrefu, tena hadharani limekuwa likihusishwa na Real Madrid.

Sancho kwa upande wake, amekuwa akihusishwa pia na dili la pesa nyingi na klabu ya Ligi Kuu England, akiripotiwa kutaka kurejea Old Trafford miaka kadhaa baada ya kuachana na Manchester City na kwenda kutamba Borussia Dortmund.

Wachezaji hao wawili wanaweza kupishana mlangoni Old Trafford, lakini wana mambo yanayofanana baada ya utoto wao wote wote kukuzwa na klabu za England kabla ya saini zao kuhitaji pesa ndefu.

Pogba aliigharimu pesa iliyovunja rekodi ya dunia aliporejea Old Trafford akitokea Juventus, wakati huo Mashetani Wekundu wakiwa tayari kulipa pesa nyingine nyingi kumnasa Sancho.

Kocha wa zamani wa Arsenal, Wenger alisema kwamba haya mambo hayaingii kabisa akilini. “Unanunua kwa pesa nyingi mchezaji ambaye ulimfundisha mwenyewe. Hivyo ni vitu vinavyochanganya, haviingii akilini,” alisema.