Gaucho arudi Simba Queens
BAADA ya vita ya muda mrefu kati ya Simba Queens na Yanga Princess juu ya mshambuliaji wa Twiga Stars, hatimaye Simba imeshinda vita hiyo na imefanikiwa kuinasa saini ya Mwanahamisi Omary 'Gaucho' na kumsainisha mkataba wa miaka miwili.
Gaucho ambaye amevunja mkataba wake na waajiri wake wa zamani Mohammadia inayoshiriki Ligi Kuu ya Wanawake nchini Morocco, amejiunga Simba kwa mara ya pili baada ya awali kuichezea kabla ya kwenda Morocco.
Mwanaspoti inafahamu kwamba Yanga Princess pia ilikuwa inahitaji sana huduma ya fundi huyu na ilishaweka ofa mezani lakini wawakilishi wa mchezaji huyo waliikataa ofa hiyo kwa sababu ilionekana kuwa ndogo ukilinganisha na ile ya Simba.
Vigogo wa Simba walipambana kumpata straika huyo ili kuboresha kikosi chao ambacho kimeonekana kuanza vibaya Ligi Kuu ya Wanawake nchini (WPL) hali inayotishia nafasi yao ya kutetea ubingwa.
Simba Queens inashika nafasi ya nne baada ya kucheza mechi tano, ikishinda tatu, sare moja na kufungwa moja hivyo kukusanya pointi 10.
Wakati anaondoka Tanzania nyota huyu alikuwa amechukua mataji matatu ya Ligi Kuu ya Wanawake mara mbili akiwa Simba na mara moja akiwa na Mlandizi Queens (2016).