Erick Mwijage ailiza Simba kipindi cha kwanza kwa Mkapa

WANANDUGU Yusuph Mhilu (winga wa kulia) na mdogo wake Dickson (beki wa pembeni) leo wameanza katika kikosi cha Kagera Sugar, inayocheza dhidi ya Simba kwenye uwanja wa Mkapa, Dar es Salaam mchezo wa Kombe la Shirikisho la Azam (ASFC).

Mhilu anayeongoza kwa ufungaji katika timu hiyo (mabao 7) ameonekana kupambana kufika langoni mwa Simba akitokea pembeni, lakini uimara wa Mohamed Hussein 'Tshabalala' umemnyima uhuru wakuzitikisa nyavu.

Kama Isingekuwa Uwanja wa Benjamin Mkapa kuwa na majimaji huenda makali yake yangeweza kuonekana kwa uwazi zaidi.

Kwa upande wa mdogo wake Dickson naye alikuwa anapambana kuwakaba mawinga, wakati mwingine mabeki wa Simba wakipanda kushambulia.


DAKIKA 45 ZA KIPINDI CHA KWANZA

Hakuna timu ambayo ilionyesha changamoto dhidhi ya nyingine, kutokana na changamoto ya Uwanja wa Benjamin Mkapa kuwa na majimaji yaliotengeneza tope.

Mechi ilikuwa ngumu, huku kila timu ikipambana kupata bao, ambapo Kagera Sugar imefanikiwa kuifumua Simba dakika ya 44.

Bao la Kagera Sugar limefungwa na Erick Mwijage, baada ya wachezaji wa timu hiyo kupigiana pasi wakiwa eneo la Simba, ndipo mchezaji huyo alipoamua kufanya maamuzi ya kupiga shuti lililomshinda Aishi Manula.