Dante, Kijibwa hatihati kuwakosa Azam FC

Dante, Kijibwa hatihati kuwakosa Azam FC

NYOTA wa kikosi cha KMC, Andrew Vicent 'Dante', Abdul Hilary 'Kijibwa' pamoja na Keneth Masumbuko huenda wakaukosa mchezo wa kesho dhidi ya Azam FC.

KMC na Azam zinakutana kesho saa 10:00 jioni mchezo utakaopigwa katika uwanja wa Uhuru, huku timu zote zikihitaji ushindi wajiweke katika nafasi nzuri.

Kupitia taarifa iliyotolewa na Afisa Habari wa klabu hiyo,Christina Mwagala imeeleza kuwa katika kikosi chao kina majeruhi watatu mpaka sasa.

"Tuna majeruhi watatu lakini katika mchezo huo tutahakikisha tunacheza mpira spana na hakutokuwa na mpira ice cream wala Strowbeli."

Mwagala amesema timu yao imejipanga kuhakikisha kwamba licha ya wapinzani wao kuongoza ligi kuu,maandalizi yaliyofanyika kwao chini ya Kaimu Kocha Mkuu, John Simkoko pamoja na kocha msaidizi Habibu Kondo yataleta matokeo mazuri.

"Katika kipindi chote cha mapumziko ,KMC FC ilitumia nafasi ya kucheza mechi nyingi za kirafiki na hivyo kutoa nafasi kwa walimu kurekebisha makosa mbalimbali ambayo yalionekana katika michezo hiyo na kwamba mashabiki wategemee kupata alama tatu katika mchezo huo".