Hello

Your subscription is almost coming to an end. Don’t miss out on the great content on Nation.Africa

Ready to continue your informative journey with us?

Hello

Your premium access has ended, but the best of Nation.Africa is still within reach. Renew now to unlock exclusive stories and in-depth features.

Reclaim your full access. Click below to renew.

Coastal Union yaanza na kiungo wa boli

KIUNGO Pict

Muktasari:

  • KenGold, imeshuka daraja na msimu ujao itashiriki Ligi ya Championship kutokana na kutokuwa na mwenendo mzuri hadi sasa, ikiburuza mkiani na pointi zake 16, baada ya kushinda mechi tatu, sare saba na kupoteza 17 kati ya 27 ilizocheza.

WAGOSI wa Kaya, Coastal Union wameanza usajili wa kimya kimya kwa kuibomoa Ken Gold kwa kuamua kumsajili kiungo Kiala Lassa wa timu hiyo iliyoshuka daraja, ikiwa ni maandalizi ya msimu mpya wa 2025-26.

KenGold, imeshuka daraja na msimu ujao itashiriki Ligi ya Championship kutokana na kutokuwa na mwenendo mzuri hadi sasa, ikiburuza mkiani na pointi zake 16, baada ya kushinda mechi tatu, sare saba na kupoteza 17 kati ya 27 ilizocheza.

Licha ya timu kuwa na hali mbaya, Kiala ameonekana kuwa chaguo muhimu ndani ya kikosi cha Coastal Union ambayo tayari imeanza mazungumzo naye huku ikielezwa kuwa mwisho wa msimu atakuwa mchezaji huru kutokana na mkataba aliosaini na timu hiyo.

Taarifa za ndani ambazo Mwanaspoti imezipata zinaeleza Coastal Union imeshaanza mazungumzo na kiungo huyo na wamefikia hatua nzuri kinachosubiriwa ni kiungo huyo kumaliza msimu.

“Mazungumzo kwa pande zote mbili yanakwenda vizuri kinachosubiriwa ni mchezaji mwenyewe kusaini mkataba na tunaamini mambo yatakwenda kama tulivyopanga,” alisema mtoa taarifa huyo ambaye hakutaka jina lake litajwe.

Kwa upande wa kiungo huyo Mkongomani, alipotafutwa na Mwanaspoti kuhusiana na kutua Coastal Union, alisema kwa sasa ni mapema kuzungumzia hilo, kwa sababu bado ni mchezaji wa KenGold huku akisisitiza kuwa mwisho wa msimu mambo yatawekwa wazi.

“Ni mapema sana kuzungumzia mambo ya kusaini timu nyingine nikiwa bado nina mechi tatu mkononi, timu kushuka haina maana kwamba kila kitu kimekamilika bado tuna michezo mitatu ambayo matamanio ni kuona tunashinda yote ili tushuke kwa heshima,” alisema.