Chukwu amtaja Aziz KI, afunguka dili la Yanga

Muktasari:

  • Kiungo huyo aliwavutia mabosi mbalimbali wa klabu nchini baada ya kuonyesha kiwango bora alipokuja na timu yake ya zamani Rivers United kwenye michuano ya Kombe la Shirikisho (CAF).

MORICE Chukwu ni majina ambayo yalitikisa wakati wa dirisha dogo la usajili akihusishwa na timu mbalimbali nchini ikiwemo Yanga lakini baadae akaibukia Singida Big Stars na sasa Ihefu.

Kiungo huyo aliwavutia mabosi mbalimbali wa klabu nchini baada ya kuonyesha kiwango bora alipokuja na timu yake ya zamani Rivers United kwenye michuano ya Kombe la Shirikisho (CAF).

Mwanaspoti hivi karibuni lilifanya mahojiano na mchezaji huyo kwanza kujua kuhusu ligi ya Tanzania na dili lake la Yanga liliishaje.


LIGI KUU

Anasema ligi ya Tanzania imekuwa na ushindani na kukua siku hadi siku jambo ambalo linawavutia baadhi ya wachezaji wa nje kucheza kutokana na mvuto wa aina yake.

“Nina furaha kucheza ligi ya Tanzania ina ushindani wa aina yake japo ilikuwa ngumu kwangu wakati nafika, lakini kwa sasa nimeanza kuzoea mazingira,” alisema Chukwu.


KUHUSU DILI LA YANGA

Msimu uliopita Yanga iliitoa Rivers United robo fainali Kombe la Shirikisho Afrika kwa jumla ya mabao 2-0 na tetesi zilidai Chukwu alikuwa akitajwa kujiunga na Yanga baada ya kuonyesha kiwango bora na hapa anajibu.

“Hata mimi nilichanganyikiwa kuhusu hilo, nilijua naenda Yanga lakini ghafla ikageuka ndipo nilifanya uchaguzi wangu binafsi baada ya Singida kunifuata na kutaka huduma yangu.”


NGAO YA JAMII ALIINJOI

Mechi ya ngao ya jamii dhidi ya Simba iliyochezwa Agosti 10 mwaka jana Uwanja wa Mkwakwani ambayo Singida ilitolewa kwa mikwaju ya penati 4-2 dakika 90 zikiisha kwa suluhu, anasema ilikuwa mechi bora kwake.

Anasema alifurahi kucheza mechi hiyo ambayo ilikuwa ya kwanza kwake tangu atue nchini akitokea Rivers United ya Nigeria.

“Ilikuwa mechi ngumu kwangu kwa kuwa ndio ilikuwa ya kwanza kucheza na Simba, nilifurahi sana, kubwa zaidi nilifunga bao dakika ya tano na mwamuzi akakataa,” alisema.


WATATU FRESHI

Marouf Tchakei, Joash Onyango, Duke Abuya wakiwepo uwanjani anafurahi kucheza nao kama timu kwa kuwa ni wachezaji wazuri na wana uzoefu.

Ukiachana na hao watatu ambao anacheza nao Singida Black Stars (Ihefu) anamtaja kiungo mshambuliaji wa Yanga, Stephane Aziz KI na Fiston Mayele ambao akicheza nao anainjoi.

“Niliwahi kucheza na Mayele kabla hajaondoka kwenda Pyramids FC ya Misri na Aziz KI ambao nilikutana nao kwenye Kombe la Shirikisho Afrika (CAF) hatua ya robo fainali ni wachezaji wazuri.”


KOKOTE SAWA

Anasema namba yoyote anacheza uwanjani kulingana na Kocha atakavyompanga na kumpa majukumu kwa siku hiyo.

“Nacheza kama kiungo mkabaji muda mwingine kama kiungo mshambuliaji, ndiyo namba ninazocheza sana lakini kokote kocha atakaponipa nafasi ya kucheza natimiza majukumu yangu.”


KUHUSU CHAKULA

Kulingana na madaktari wanavyoshauri mlo wa wachezaji hawapaswi kula sana kuna baadhi ya vyakula wanakula na vingine hawatumii kabisa au wanapunguza.

“Mimi sio mlaji sana kwa kuwa wataalamu wanatupa angalizo na ushauri wa lishe ili uweze kucheza vizuri lakini kwa vyakula vya Tanzania napenda pilau na ugali.”


WAZAWA

Anawataja wachezaji watatu wazawa ambao wanamfurahisha wanapokuwa uwanjani akiwemo beki wa kati wa Yanga, Ibrahim Bacca, kiungo mkabaji wa Singida Big Stars, Yusuph Kagoma na kipa Ibrahim Parapanda.

“Bacca ni beki mzuri ukitaja majina ya walinzi Tanzania, napenda namna anavyojiamini kipa wetu Parapanda na Kagoma wapo wengi lakini hao ni wazuri zaidi.”