Biashara yaisikilizia CAF

Timu ya Biashara inasubiri tamko la Shirikisho la Soka la Afrika (CAF) ili kujua hatma ya mechi yake ya Shirikisho dhidi ya Al Ahly Tripoli ya Libya.

Mechi hiyo ilipangwa kucheza leo nchini humo na hadi saa 6 mchana Biashara United ambayo iko kambini Dar es Salaam haikuwa na uhakika wa safari.

Rais wa Shirikisho la Soka Tanzania ( TFF), Wallace Karia ameiambia Mwananchi Digital kwamba bado wanasubiri taarifa ya CAF juu ya ombi la kusogezwa mbele mchezo huo hadi Jumanne.

"Tunasubiri majibu ya CAF ili kuona kama timu itasafiri au vinginevyo," amesema Karia.

Haji Mtete wa Biashara amesema changamoto ilianza kwa kukosa bima.

"Kabla ya kupata ndege ya ATCL ambayo changamoto yake ilikosa vibali, tulikodi ndege awali tangu Oktoba 17, tukakwama kwenye bima," anasema Mtete.

Anasema ugumu wa safari yao ulianza kuonekana mapema baada ya ndege ya abiria kwenda nchini humo kuwa changamoto.

"Ni kweli Biashara tuna changamoto ya pesa, lakini pia na nchi ambayo tunatakiwa kwenda inachangamoto hasa kwenye usafiri, ndege ya abiria tulikosa, ya kukodi pia tulikwama kupata bima,".

Anasema kwenye ndege ya ATCL ilikubali kwenda, changamoto imekuwa ni kibali cha kupita kwenye anga ya kimataifa nchini Sudan, Sudan Kusini na cha kutua Benghazi utakapochezwa mchezo huo.

"Mchakato wa kuomba vibali unaendelea wakati huo huo tukisubiri uamuzi wa CAF, wakikubali tutasafiri, ikishindikana basi hatutakuwa na namna nyingine," amesema.