Azam yaishusha Geita Gold

Azam yaishusha Geita Gold

WINGA wa Azam FC, Ayubu Lyanga ameendeleza ubabe mbele ya kipa  wa Mtibwa Sugar, Jeremiah Kisubi akicheka na nyavu dakika ya 20 na 54.
Lyanga alikuwa kwenye kiwango kizuri, kilichowapa kazi ngumu mabeki wa Mtibwa  kumdhibiti asiendelee kuleta madhara langoni mwao.

Ukuta wa Azam ukiongozwa na mkongwe Agrey Morris uliimarishwa na kuwapa tabu washambuliaji wa Mtibwa Sugar kupenya katikati yao, hivyo mashambulizi yao yalikuwa yanaanzia pembeni.

Hata hivyo kiungo fundi wa Mtibwa Sugar, Said Ndemla alipambana kutoa krosi nzuri ambazo hazikuwa zinatendewa haki na wale aliokuwa anawatengenezea.

Ndemla alijaribu kupiga mashuti ya mbali mara kwa mara, akafanikiwa kumtungua kipa wa Azam dakika ya 80 na kuipa Mtibwa bao la kufutia machozi.

Hata hivyo Ndemla ameonekana kucheza kwa kutumia akili zaidi kwa kupiga mashuti maeneo yasiyotegemewa akikwepa ulinzi wa Azam.

Kwa matokeo hayo Azam imepanda hadi nafasi ya nne ikiwa na pointi 36 ikiishusha Geita Gold nafasi ya tano ikiwa na alama 34.