Azam FC, Gor Mahia kinapigwa
Muktasari:
- Azam inakwenda kucheza mechi hiyo ikiwa ni moja ya maandalizi ya mchezo ujao wa Ligi Kuu Bara dhidi ya Mtibwa Sugar utakaochezwa Novemba 24, kwenye Uwanja wa Azam Complex jijini Dar es Salaam.
AZAM FC inatarajia kucheza mechi ya kirafiki ya kimataifa dhidi ya mabingwa watetezi wa Ligi Kuu Kenya (FKF-PL), Gor Mahia, jijini Nairobi, Novemba 19.
Azam inakwenda kucheza mechi hiyo ikiwa ni moja ya maandalizi ya mchezo ujao wa Ligi Kuu Bara dhidi ya Mtibwa Sugar utakaochezwa Novemba 24, kwenye Uwanja wa Azam Complex jijini Dar es Salaam.
Ofisa Habari wa Azam FC, Thabit Zacharia ‘Zaka Zakazi’ alisema timu hiyo ilikuwa na mpango wa kucheza na mabingwa hao tangu msimu uliopita, lakini walishindwa kutokana na hali ya kisiasa iliyokuwepo wakati huo.
Alisema hivi sasa ni muda muafaka kucheza na Gor Mahia kwani ni timu ambayo itawapa kipimo sahihi.
“Unajua timu zote ambazo tungetaka kucheza nazo hapa ni zilezile tunazokutana nazo kwenye ligi, hivyo kusingekuwepo na tofauti yoyote ndiyo maana tumeona tucheze na Gor Mahia mechi ambayo itakuwa na tofauti kubwa,” alisema Zaka.
“Timu itaondoka Novemba 18, siku itakayofuata tutacheza mechi na baada ya mechi tutarudi (nchini) kuendelea na maandalizi ya mwisho ya kucheza na Mtibwa Sugar.”