Aubameyang achefua watu rangi za magari yake

Muktasari:

Mashabiki wake wamelichukulia suala hilo kuwa ni uharibifu tu wa pesa.

LONDON, ENGLAND.STRAIKA wa Arsenal, Pierre-Emerick Aubameyang ameingia kwenye lawama kubwa akishutumiwa kufanya matumizi mabaya ya pesa baada ya kuamua kulipiga rangi ya hovyo gari lake la kifahari la Ferrari lenye thamani ya Pauni 2 milioni.

Fowadi huyo wa kimataifa wa Gabon aliamua kwenda kupiga rangi tofauti ya kumelemeta gari lake hilo, wakati mwonekano wa awali ulikuwa bora zaidi.

Mashabiki wake wamelichukulia suala hilo kuwa ni uharibifu tu wa pesa.

Staa Aubameyang alitaka gari lake hilo liwe na mwonekano tofauti, hivyo hata linapopita barabarani au kuwa kwenye maegesho, basi iwe rahisi kuonekana kama wanavyofanya wanasoka wanapokuwa uwanjani, ambapo wengine wamekuwa wakipaka nywele rangi au kuweka mitindo tofauti kujitofautisha na wenzao.

Hata hivyo, hiyo si mara ya kwanza kwa Aubameyang kuzibadili rangi gari zake za kifahari baada ya kuwahi kufanya hivyo kwa ndinga zake nyingine za Lamborghini Aventador, Range Rover Sport na Lamborghini Urus.

Mwenyewe anafahamu kwamba hicho anachokifanya kina sura mbili, kuna watakaokipenda na kuna wengine watakichukia.