Amrouche awavimbia Waganda

Muktasari:

  • Amrouche alisema licha ya kuwa na muda mchache wa maandalizi amefurahia uwajibikaji wa mchezaji mmoja mmoja na morali ya timu kwa ujumla.

KOCHA wa Taifa Stars, Adel Amrouche ameeleza namna ambavyo kikosi chake kipo tayari kwa mchezo wa kuwania nafasi ya kufuzu kwa ajili ya fainali za mataifa ya Afrika  dhidi ya Uganda huku akiamini nyota wake wanaweza kuwapa raha Watanzania.

Amrouche alisema licha ya kuwa na muda mchache wa maandalizi amefurahia uwajibikaji wa mchezaji mmoja mmoja na morali ya timu kwa ujumla.

"Hatuna sababu ya kusingizia, hii ni timu na tunapaswa kuwapa furaha Watanzania, siku zote nimekuwa kocha mwenye mtazamo chanya hivyo naamini kuwa tunaweza kupambana na kupata matokeo mazuri kwa sababu tunao wachezaji wenye ubora na hata uzoefu,"

"Tumekuwa na maandalizi mazuri ambayo yamejikita kwenye mbinu juu ya namna ya kucheza na kupata matokeo, tunapaswa kufanya kazi kwa pamoja," alisema kocha huyo.

Amrouche aliongeza kwa kusema, "Nitafurahi kuona tunafanya vizuri kwenye michezo yote miwili dhidi ya Uganda na sote tunafahamu walivyo na timu ngumu na shindani,"

Mara baada ya kumalizana na Uganda hapo leo, Ijumaa vijana wa Amrouche watarejea nyumbani Tanzania kwa ajili ya kibarua kingine cha marudiano  dhidi ya The Cranes Jumanne ya Machi 28.