Alichosema Barbara baada ya kipigo cha ASEC

HAKUNA kulaumiana, hiyo ni kauli ya Mtendaji Mkuu wa Simba, Barbara Gonzalez baada ya kukubali kipigo cha mabao 3-0 dhidi ya ASEC Mimosas jana.
Simba jana alikuwa mgeni wa Mimosas mchezo uliopigwa nchini Benin baada ya viwanja vya Ivory Coast kuwa katika matengenezo kwa ajili ya michuano ya Afcon.
Barbara amesema kuwa, sio wakati wa kulaumiana sasa wala kunyoosheana vidole kwa matokeo hayo bali ni kujipanga kwa ajili ya mchezo wa mwisho dhidi ya US Gendarmerie.
"Tunatakiwa tujipange kwa ajili ya mchezo wa mwisho, kwani bado tuna nafasi ya kutinga hatua ya robo fainali kama tutashinda na US kwa hiyo hatupaswi kupoteza lengo," amesema Barbara.
Katika harakati za kufikia lengo Mtendaji huyo amesema, baada ya kurejea kesho wachezaji wote Machi 27 watatakiwa kurejea mazoezi na kuanza kambi ya kuelekea mchezo huo.
Simba katika kundi lao ina pointi saba sawa na RS Berkane huku ASEC Mimosas wao wakiwa vinara kwa pointi tisa huku US wakiburuza mkia pointi tano pekee.