Siku 52 za Dejan Simba, kisa cha kuondoka

Siku 52 za Dejan Simba, utata wa kuondoka

Muktasari:

  • Mshambuliaji wa Simba, Dejan Georgijevic imemchukua siku 52, kuishi kwenye kikosi hicho tangu alipotambulishwa Agosti 7, hadi jana alipositisha mkataba wa kuitumikia timu hiyo kutoka na sababu kubwa tatu.

Dar es Salaam. Mshambuliaji wa Simba, Dejan Georgijevic imemchukua siku 52, kuishi kwenye kikosi hicho tangu alipotambulishwa Agosti 7, hadi jana alipositisha mkataba wa kuitumikia timu hiyo kutoka na sababu kubwa tatu.

Dejan aliandika ujumbe katika mtandao wa kijamii uliyoeleza: “Nathibitisha kuwa mkataba wangu na Simba umevunjika, kutokana na muajiri wangu kukiuka makubaliano ya kimkataba, asante mashabiki kwa mapenzi yenu.”

Baada ya ujumbe huo wa jana asubuhi, Dejan alikutana na wachezaji wenzake kambini kuagana nao na alifanya hivyo kwa benchi la ufundi alilofanya nalo kazi chini ya kocha wa mpito, Juma Mgunda.

Nyota huyo aliondoka kambini kwenda Bandarini kwa ajili ya kurejea Dar es Salaam alikofika saa 8:30 mchana kisha alikwenda ofisi za Simba kukamilisha taratibu zake za kumalizana na timu hiyo ili kutimka nchini.


Utata wa kuondoka

Inaelezwa kuwa tangu alipofika nchini Agosti 7, Dejan alikuwa akiishi katika moja ya hoteli kubwa iliyopo Mbezi, na hakupata nyumba ya kuishi ile aliyokuwa hakiitaji.

Uongozi wa Simba ulipambana na kumpatia nyumba mbalimbali ila mchezaji huyo alikuwa akizikataa kwa madai kuwa si za kumfaa kuishi.

Inadaiwa kuwa pia Dejan alifikia uamuzi huo kutokana na kushindwa kupata baadhi ya stahiki zake walizokubaliana na uongozi wa Simba wakati akisaini mkataba wa kuitumikia. Miongoni mwa maslahi hayo ni mshahara wake, bonansi pamoja na fedha ya usajili.

Sababu nyingine inayodaiwa kuchangia kusitisha mkataba wake ni kuwepo na baadhi ya mambo yaliyokuwa yakiendelea ndani ya timu na hakupendezwa.


Alichosema Dejan

Mara baada ya kurejea Dar es Salaam, jana mchana, Dejan aliliambia gazeti hili kwamba si vyema kuweka wazi sababu zilizochangia kufanya uamuzi ila kuna mambo hayakwenda sawa kwenye makubaliano yao ya mkataba.

Dejan alisema kuna vitu alikubaliana na uongozi na kuelezwa atapatiwa ila kadri muda ulivyozidi kwenda aliona hakuna ambalo limetimizwa.

Alisema Simba ni timu kubwa Afrika, si vyema kuweka wazi mambo hayo ila ndiyo vitu vikubwa vilivyochangia kufanya maamuzi ya kurudi kwao Serbia kwa ajili ya kujipanga kabla ya kuanza maisha mengine.

“Maisha ya soka ndivyo yalivyo kuna uamuzi mgumu lazima ufanyike kwa ajili ya hatma ya maisha yangu nawapa pole mashabiki wa Simba, naipenda timu hii ila ilikuwa haina jinsi,” alisema.


Siku 52 Simba

Katika siku hizo 52, ambazo Dejan alikuwa kwenye kikosi cha Simba, timu yake ilicheza mechi saba za kimashindano Ngao ya Jamii, Ligi Kuu Bara mechi nne na mbili za Ligi ya Mabingwa Afrika.

Katika michezo hiyo ya kimashindano, Dejan alicheza minne hakuna hata mmoja ambao alianza kikosi cha kwanza na yote alikuwa akiingia kipindi cha pili.

Jumla ya dakika alizocheza katika michezo yote minne ni 70, licha ya kuwa kipenzi cha mashabiki wengi wa Simba nchini.

Katika Ligi Kuu Bara Dejan alifunga bao moja kwenye mchezo dhidi ya Kagera Sugar, ambao Simba ilishinda mabao 2-0, lingine likifungwa na Moses Phiri.