Ajib mpya sasa ampa mzuka Sven

Ajib mpya sasa aamsha mzuka Simba

IBRAHIM Ajib amekuwa na mabadiliko makubwa kwenye siku za karibuni mazoezini ambayo yamemshangaza Kocha Sven Vandebroeck, ambaye ameahidi kumpa nafasi.

“Tangu katika maandalizi ya ligi Ajibu alionyesha kuna kitu anahitaji katika mazoezi, anajituma na kuonYesha ushindani kwa wenzake ambao haukuonekana mara kwa mara kwake,” alisema.

“Sasa anaonekana kufanya mazoezi vizuri. Ni jambo la kuridhisha na kama kocha, mchezaji yeyote yule anayefanya vyema, unampatia nafasi ya kucheza na nimefanya hivyo katika baadhi ya mechi na amedhihirisha licha ya kucheza vizuri amefunga bao katika mechi na Mwadui,” alisema.

“Hata katika mechi ya kirafiki na African Sports, Ajibu alikuwa mmoja wa wachezaji ambao niliwafunga GPRS ili kuona wamekimbia na wametumika kwa kiasi gani jambo ambalo alivuka kile kiwango ambacho nilitarajia kutoka kwake.

“Sio Ajibu tu ambaye ameonyesha kuwa anatamani kuaminiwa na kucheza bali hata Kennedy Juma na Ibrahim Ame nao wamekuwa wakijituma na kuonyesha katika mazoezi na hata mechi ya kirafiki na African Sports walikuwa katika viwango bora,” aliongeza Sven.

“Kikubwa wachezaji waliokuwa katika majukumu ya timu zao za taifa wengi wamerejea na tumeanza mazoezi ya pamoja,” alisema.


SVEN KUSHUSHA KIUNGO MPYA

Sven alisema tayari wameanza mchakato wa kutafuta wachezaji wapya na mapendekezo yake ya kwanza anataka asajiliwe kiungo mwenye uwezo wa kukaba.

Sven alisema baada ya kumkosa Gerson Fraga ambaye wameachana naye kutokana na majeraha, moja kwa moja ni pengo kwao kwa maana hiyo ameingia sokoni kutafuta kiungo mkabaji kwenye timu na nchi tofauti ingawa habari za ndani zinasema yumo Mzimbabwe.

“Nitawaomba viongozi wamnunue mmoja ambaye atakuwa na uwezo na kuja kuziba nafasi ya Fraga,” alisema Sven.

______________________________________________________________

Na THOBIAS SEBASTIAN