Prime
Rafiki yetu Xabi Alonso, ndoa ilikufa kabla haijafungwa
HADITHI nyingine zinachekesha sana. Hizi hadithi za mpira zinachekesha sana. Siku moja katika uwanja wa mazoezi wa Bayern Munich, Sabener Strabe, kocha wao wa zamani, Louis Van Gaal aliwahi kushusha suruali yake na kuonyesha utupu wake kwa kiungo staa wa Bayern wa wakati huo, Bastian Schweinsteiger.
Alikuwa anamwambia kwamba yeye ni mwanaume haswa. Labda ilitokea dharau ya hapa na pale kati yao, lakini Van Gaal akamwambia Bastian kwa vitendo kwamba yeye alikuwa mwanaume haswa. Akavua alichovaa na kumuonyesha utupu wake.
Maisha sio rahisi kwa makocha. Fikiria namna ambavyo Pep Guardiola alipofika kwa mara ya kwanza katika uwanja wa mazoezi wa Barcelona, Ciutat Esportiva Joan Gamper na kuwaambia Ronaldinho Gaucho na Decop de Souza kwamba hawakuwa katika mipango yake. Dunia iliachwa midomo wazi.
Msimu mmoja baadaye akamwambia Samuel Etoo lugha hiyo hiyo. Kwamba hamtaki. Kumbuka kwamba watatu hawa walikuwa wameishika Barcelona. Ni kama kilichokuja baadaye kwa Xavi Hernandes, Lionel Messi na Andres Iniesta. Lakini nani angeamini ambacho kingekuja wakati kina Ronaldinho wanaondolewa? Hakuna.
Rafiki yangu au niseme rafiki yetu, Xabi Alonso ameachana na Real Madrid mwanzoni mwa wiki hii. Kwangu ni ndoa ambayo ilivunjika kabla haijaanza. Nimelazimika kukumbuka mifano ya kina Van Gaal na Pep baada ya kufukuzwa.
Mambo ni mengi na muda ni mchache. Kama Van Gaal alimfanyia vile Bastian ni kwa sababu rekodi ya Van Gaal kama kocha ilikuwa nene haswa na ikamtengenezea kiburi kikubwa. Alonso asingeweza kuwa na kiburi chochote kwa mchezaji yeyote mkubwa wa Real Madrid.
Kwa upande wa Pep nadhani alifanya hivyo kwa sababu aliamini katika falsafa yake, lakini pia alikuwa katika timu ambayo iliamini katika soka la vijana na ndio maana ikatengeneza shule nzuri kubwa ya soka iliyotamba na inayoendelea kutamba duniani, La Masia.
Tatizo lilikuja kwa Alonso pale Real Madrid. Alifanya vyema na Bayer Leverkusen. Aliwamiliki vyema wachezaji wa Bayer Leverkusen ambao wengi hawakuwahi kufikia ukubwa wa jina lake wakati anacheza soka. Wengi walimtii na wakacheza kama punda.
Kumtoa Bayern Munich kileleni pale Ujerumani sio jambo la masihara sana, lakini Alonso alifanya. Alikusanya vijana wake wanaomtii na wakamfanyia kazi ya kushangaza. Kwa mara ya kwanza katika historia ya Bundesliga, Bayer Leverkusen wakatwaa taji Ujerumani.
Kuhamishia kitu kama hiki pale Santiago Bernabeu ilikuwa ni ndoto ya mchana. Unakutana na Kylian Mbappe ambaye ameshawahi kutwaa Kombe la Dunia na mataji ya Ufaransa akiwa na PSG mara nyingi tu. Unakutana na kina Vinicius Junior ambao wanajiona kuwa ni wanasoka bora wa dunia baada ya Cristiano Ronaldo na Lionel Messi. Ni kazi ngumu.
Tunakumbuka namna ambavyo msimu huu huu Alonso alimuita nje Vinicius na kijana huyo Mbrazili akarusha mikono juu katikati ya uwanja kuonyesha kutoridhika, na pia kumtangazia ubaya Alonso kwa mashabiki. Hakuna mchezaji wa Leverkusen ambaye angeweza kufanya hivyo kwa Alonso.
Ukiachana na hiyo timu yake ya zamani, hata sasa hakuna mchezaji wa Manchester City anayeweza kumfanyia hivyo Pep Guardiola wala hakuna mchezaji wa Arsenal anayeweza kumfanyia hivyo Mikel Arteta. Makocha wamewaweka mfukoni wachezaji na wameonyesha mamlaka yao.
Tukiachana na hilo, kuna klabu zina falsafa zao ambazo zingeendana na Alonso. Real Madrid sio mojawapo. Real Madrid wana biashara zao wanachanganya na majina ya wachezaji wakubwa. Kuna klabu nyingine zinaweza kumudu makocha ambao hawapo bize na biashara za klabu.
Alonso alihitaji klabu ambayo wachezaji wangetumikia mfumo wake na si kuangalia sana masuala ya kibiashara. Mfano ni namna ambavyo ghafla alitokea kumuamini kinda wa Kituruki, Arda Guller. Bila kujali ni kwa gharama ya nani angekaa nje, Alonso aliamini zaidi katika Arda Guller.
Unajenga timu kwa misingi ya nidhamu na uwajibikaji. Unajenga timu kwa msingi ya kitimu zaidi kuliko kuangalia biashara za nje ya uwanja. Unajenga timu yenye umoja ndani na nje ya uwanja. Ndio maana Pep aliachana na kina Ronaldinho.
Alijua tu kwamba kina Ronaldinho licha ya vipaji vyao vikubwa, lakini wasingemtii sana ndani na nje ya uwanja. Ndani ya uwanja Ronaldinho asingeweza kukaba katika kiwango cha juu wakati akiwa hana mpira.
Messi na Iniesta walikuwa wanafanya hivyo kwa kiwango cha hali ya juu. Hata alipokwenda Manchester City, Kevin De Bruyne licha ya uwezo wake mkubwa uwanjani lakini alimudu kufanya hivyo.
Nje ya uwanja alijua kwamba kina Ronaldinho walikuwa wanakesha katika klabu za usiku katikati ya Jiji la Barcelona wakiwa na warembo. Wangewezaje kucheza staili ya mpira aliokuwa anataka kuuanzisha Barcelona kama wangeendelea na maisha hayo? Akaamua kuanza upya na kuingiza staili ya soka ambayo leo inaabudiwa duniani. Unakabia kuanzia juu na kila mahala.
Hata Mikel Arteta aliamua kuachana na kina Mesut Ozil na Pierre-Emerick Aubamayeng kwa sababu alijua ndani na nje ya uwanja wasingempa ambacho alikuwa anakitaka. Alilaumiwa wakati ule lakini Arsenal ya leo ni bora kuliko wakati wakiwa na watu wale wawili.
Ingekuwa ngumu kwa Alonso kutimiza ndoto zake Real Madrid kwa sababu falsafa kama hizi za kocha haziwezi kukubalika kwa Real Madrid. Rais Florentino Perez ana biashara zake anazifanya kupitia kwa wachezaji wake mastaa. Hauwezi kumuambia kwamba leo Arda Guller ni muhimu katika timu kuliko Vinicius.
Lakini pia kwa mashabiki wa timu hii sidhani wana muda na kitu ambacho kinachoitwa ‘project’. Kwamba wakupe miaka mitatu ya kusuka timu huku ukiwa unayumbayumba. Sidhani kama ni kitu ambacho wanaweza kukubali.
Bahati mbaya kwa Alonso ni kwamba wakati akiendelea kusuka mambo timu ilikuwa inasuasua. Na mpaka sasa hakuna kinachoeleweka kati yao. Kuna vyombo vya habari vya Hispania vinadai kwamba Alonso aliamua kuondoka mwenyewe baada ya kuona asingeweza kufanya kazi katika mazingira hayo magumu.
Wengine ndio ambao wanaripoti kwamba Real Madrid waliamua kuachana na Alonso. Yote hayo yanawezekana kama ukichunguza namna ndoa hii ilivyoundwa. Kwangu mimi nadhani ilivunjika kabla haijaundwa. Kitu ambacho naweza kuweka ahadi hapa ni kwamba Alonso ataibuka na timu nyingine na itakuwa imara sana.
Akipewa timu ambayo inaweza kumvumilia kwa miaka mitatu tu na kumpa uhuru wa kila anachofanya nadhani Alonso ataendelea kuibuka kama miongoni mwa makocha mahiri wa kizazi hiki. Anaweza kupata ndoa mwafaka na timu yenye uvumilivu. Hata kama ni kubwa, lakini imuachie uhuru wa kufanya mambo yake.