Prisons wasiingie kwa mazoea dhidi ya Polisi
Muktasari:
- Mechi hizo mbili ni za hatua ya mchujo dhidi ya Polisi Tanzania ambapo kama itapoteza itashuka daraja na ikifanya vizuri itabaki Ligi Kuu.
MAAFANDE wa Tanzania Prisons wamebakisha mechi mbili za kuwabakisha Ligi Kuu vinginevyo watakwenda na maji na kushuka hadi ligi ya Championship.
Mechi hizo mbili ni za hatua ya mchujo dhidi ya Polisi Tanzania ambapo kama itapoteza itashuka daraja na ikifanya vizuri itabaki Ligi Kuu.
Tanzania Prisons ina fursa ya mwisho ya kujitetea baada ya kushindwa kufanya hivyo dhidi ya Mbeya City katika hatua ya kwanza ya mchujo kwa kufungwa jumla ya mabao 2-0.
Hii sio mara ya kwanza kwa Tanzania Prisons kucheza mechi za mchujo ili kupigania kubaki Ligi Kuu Tanzania Bara.
Hata hivyo safari hii inapaswa kujipanga vilivyo kwa vile aina ya timu wanayokutana nayo sio nyepesi hata kidogo.
Polisi Tanzania ina kikosi chenye wachezaji wazuri ambao wanaweza kukabiliana na timu ya aina yoyote ndani ya nchi hii.
Lakini pia wana kocha mzoefu, Mbwana Makata ambaye ana historia nzuri ya kupandisha timu daraja kwa nyakati tofauti.
Sisi hapa kijiweni tunatamani na tunasubiria kwa hamu mechi hiyo ya ndugu wawili kwani tunajua itakuwa ya kukata na shoka.