Prime
KAMERA
SIYO kila tabasamu linamanisha furaha, wengine kupitia uso unaotabasamu wanaficha maumivu makali yasiyoelezeka kirahisi na yanaendelea kuwatafuna ndani kwa ndani, kama anavyoeleza nyota wa zamani wa Yanga, Tariq Seif Kiakala.
Wakati anazungumza na Nyuma ya Kamera, Kiakala ambaye msimu wa 2025/26 aliichezea Polisi Tanzania Ligi ya Championship, anasimulia kisa kinachomuumiza katika kazi yake ya mpira wa miguu na kushindwa kuzitumia fursa za kwenda kucheza nje ya nchi.
Anasimulia jambo ambalo hajawahi kuzungumza popote, kuhusu wakala (ameficha jina lake) aliyesimamia dili lake la kwenda Yanga msimu wa 2019/20 akitokea Biashara United, kukatalia paspoti yake, hivyo kukwama kusafiri kwenda nje.
“Ni wakala niliyemwamini sana, alibakia na paspoti kwa sababu ya dili la kwenda nje na alipata timu katika nchi ndogo ya Bahrain iliyopo Ghuba Uajemi (Arabia) eneo la Mashariki ya Kati, hakunitajia jina la timu, alitaka niende mwenyewe na kila kitu ningekijua baada ya kufika huko,” anasema na kuongeza;
“Nilipomwambia twende wote kama wakala atakayesimamia makubaliano ya kimkataba na masilahi yangu akagoma, hivyo safari ikafia hapo na hakutaka kunisimamia tena, maisha yakaenda hadi nilipopata timu nyingine Zambia nikamwambia anipe paspoti yangu akaikatalia hadi leo.”
Anasema hakutaka kuanza mambo ya kupelekana mahakamani ama kutafuta wanasheria wa kumsaidia kuipata paspoti yake kwani aliamini kama binadamu atapata muda wa kujifikiria angeona anaharibu maisha ya mtu mwingine.
“Kusema ukweli kukosa paspoti kumenirudisha nyuma vitu vingi sana, kuna wakati natamani kwenda nje nashindwa hata nikipata ofa inakuwa ngumu kukubaliana nazo, kwani najua hakuna chochote kitafanyika.”
Anaulizwa je, wazazi wako wanasemaje katika hilo, Anajibu:
“Wazazi wangu wameniachia maamuzi mwenyewe, nasita kwenda hatua za kisheria kuna wakati najiuliza huenda Mungu kuna jambo ananiepusha nalo, ujue mpira wa miguu ni kazi inayotunza familia yangu kwa maana ya kusaidia wazazi, watoto wangu, ndugu na jamaa, halafu wakala anajua hilo na anakaa na paspoti kwa amani, hilo linatafakarisha.
Anaongeza: “Kuna wakati nilitamani nitoe tangazo la paspoti yangu kupotea ili nipate mpya, bado moyo wangu ulikuwa mzito kufanya hivyo, wengi wanaotutazama uwanjani hawajui nyuma ya dakika 90 tunazokuwepo kwenye pichi tunapitia vitu vigumu baadhi yetu.”
Nyota huyo aliyewahi kuzichezea timu mbalimbali kama Stand United, Polisi Dodoma, Mbeya City, Gen Gold anasema aliondoka Yanga kwa sababu ya masilahi:
“Nakumbuka baada ya mkataba wangu kumalizika, niliambiwa nitapewa mkataba mpya, lakini hautakuwa na pesa ya usajili, badala yake nitakuwa nachukua mshahara, sikuwa tayari na hilo kwa sababu nilikuwa na watu wanaonitegemea na kuna timu ambazo zilikuwa tayari kunipa pesa za usajili.”