Hawa wanatetea hadhi zao

INGAWA kuna baadhi ya nyota wa Simba na Yanga hawakuanza Ligi Kuu kwa kishindo, hata hivyo, kadri siku zinavyosonga na ligi ikikaribia ukingoni ukiwa mzunguko wa pili, wameanza kuonyesha maajabu na hii inaweza ikawabeba mwisho wa msimu.

Mwanaspoti limefuatilia wachezaji hao na kugundua wameanza kurejea kwa kasi mzunguko huu wa pili baada ya ule wa kwanza kuchemsha kutokana na kutokuonyesha viwango bora kushawishi makocha wao kuwaanzisha kikosi cha kwanza.


MEDDIE KAGERE - SIMBA

Misimu miwili iliyopita alikuwa tishio zaidi Ligi Kuu na kuibuka kinara wa mabao ndani ya misimu hiyo, (msimu wa 2018/19, mabao 23) na (msimu wa 2019/20, mabao 22).

Hata hivyo, baada ya ujio wa Kocha Sven Vandenbroeck aliyependa kutumia mfumo wa straika mmoja, alimtumia zaidi John Bocco na Chriss Mugalu.

Kwa sasa Kagere anaonekana kupata nafasi kutokana na kuaminiwa na Kocha Didier Gomes na akiendeleza kasi yake atamaliza kwa kishindo ligi msimu huu na kwa mabao yake 11 hadi sasa anaingia kwenye ushindani wa kiatu cha Dhahabu.


ABDALLAH SHAIBU ‘NINJA’ - YANGA

Kwenye mechi dhidi ya Biashara kwenye Uwanja wa Mkapa, alionyesha kiwango safi akiisaidia Yanga kuzima mashambulizi ya Biashara.

Atamaliza msimu vizuri kama tu akiuendeleza moto wake huo, baada ya awali kuwa akikosa nafasi au kuanzia benchi kuwapisha beki ya kati Lamine Moro na Bakari Mwamnyeto chini ya aliyekuwa kocha mkuu, Cedrick Kaze.

Kaimu kocha mkuu wa timu hiyo, Juma Mwambusi alimwanzisha Ninja dhidi ya KMC (walitoshana nguvu kwa bao 1-1) na Biashara United (Yanga ilishinda bao 1-0) akisaidiana na viungo wakabaji kama Tonombe Mukoko.


MICHAEL SARPONG - YANGA

Hadi sasa ana mabao manne na asisti mbili za mabao Yanga.

Amekuwa akisuasua mara kwa mara lakini ni wazi ni kutokana na kutokujiamini katika ufungaji.

Ameanzia mechi mbili alizochezeshwa na Kocha Mwambusi na ameoshesha bado ana uwezo na hadi mwishoni mwa msimu ataibeba Yanga.


RALLY BWALYA - SIMBA

Alijiunga na Simba akitokea Power Dynamos ya Zambia mwaka 2020, lakini hakuanza kwa kishindo. Hata hivyo kwa sasa chini ya Kocha Didier Gomes ameanza kuonyesha kiwango kizuri na mchango mkubwa na akiendelea hivyo hadi mwisho wa msimu atamaliza na moto.


FARUK SHIKHALO - YANGA

Kipa Metacha Mnata ndiye alianza kwa kishindo msimu huu, hata hivyo, Shikhalo aliibuka na kuonyesha kiwango safi kwenye michuano ya Kombe la Mapinduzi na kwa sasa ndiye

anayesimama kwenye milingoti mitatu akiwa na ubora mkubwa na ataibuka shujaa mwisho wa msimu akiuendeleza moto huu.


JOHN BOCCO - SIMBA

Nahodha wa Simba aliyekuwa akisumbuliwa na na majeraha yaliyomweka nje kwa muda. Hata hivyo, amerudi na kuanza

kufanya makubwa akiifungia bao pekee la ushindi Simba dhidi ya Mwadui FC na kufikisha idadi ya mabao 10, akiwa nyuma ya straika Kagere mwenye 11. Akiendeleza mziki wake huu, ataibuka mfungaji bora kutokana na ushindani wa mabao.