Zuchu aikaushia sherehe ya mama Diamond, sababu yatajwa
Muktasari:
- Sanura ambaye ametimiza miaka 59, aliandaliwa sherehe iliyohudhuriwa na ndugu, jamaa na marafiki pamoja na wasanii mbalimbali, huku Diamond Platnumz akiwa miongoni mwa watu waliokuwa sehemu ya tukio hilo.
Sherehe ya kumbukumbu ya kuzaliwa ya mama mzazi wa staa wa Bongo Fleva, Diamond Platnumz, Sanura Kassim iliyofanyika Julai 11 nyumbani kwake, Madale, jijini Dar es salaam imeendelea kuacha gumzo baada ya msanii Zuchu kutokuwepo kwenye tukio hilo la kifamilia.
Sanura ambaye ametimiza miaka 59, aliandaliwa sherehe iliyohudhuriwa na ndugu, jamaa na marafiki pamoja na wasanii mbalimbali, huku Diamond Platnumz akiwa miongoni mwa watu waliokuwa sehemu ya tukio hilo.
Hata hivyo, jambo lililowafanya wengi kujiuliza ni kutokuwepo kwa Zuchu, ambaye mara nyingi amekuwa akionekana sambamba na Diamond kwenye matukio muhimu ya kifamilia, ikiwemo yale yanayohusisha mama mkwe wake.
Diamond alipoingia kwenye sherehe hiyo bila Zuchu, aliulizwa sababu ya kutohudhuria kwa msanii huyo, lakini alionekana kusita kujibu na kupatwa na kigugumizi kabla ya kusaidiwa na Mbunge wa Kigoma, Baba Levo.
Baba Levo alidai Zuchu hakufika kwenye sherehe hiyo kutokana na hali ya ujauzito, alisema: “Zuchu ana mimba, ndiyo maana hajaja kwenye sherehe Mnataka aje mumkanyage tumbo?”
Kauli hiyo ya Baba Levo ilimfanya Diamond kucheka na kuibua mjadala ndani ya ukumbi, huku mashabiki wakianza kuzungumzia zaidi kuhusu taarifa hiyo iliyotolewa ghafla mbele ya Diamond.
Hata hivyo, hadi sasa Diamond Platnumz wala Zuchu hawajatoa kauli rasmi kuhusu taarifa hiyo, hivyo kinachosubiriwa zaidi ni majibu yao wenyewe kuhusu sababu ya kutokuwepo kwa Zuchu kwenye sherehe hiyo muhimu ya familia.