Stamina, Twanga, Mashauzi kupamba tamasha la biriani

Dar es Salaam. Bendi ya African Stars (Twanga Pepeta) na mwanamuziki  nyota wa taarab Isha Mashauzi watapamba tamasha la Biriani  liliandaliwa na kampuni ya vinywaji baridi ya Coca-Cola kwanza kwenye viwanja vya Posta, Kijitonyama kesho Jumamosi.

Mbali ya Twanga Pepeta na Isha, tamasha hilo pia litapambwa na wasanii wa kizazi kipya ambao ni Weusi, Baba Levo, Baddest, Dulla Makabila, Stamina na Dj D Ommy  ambaye ataendesha tamasha hilo.

Meneja biashara na masoko wa Coca-Cola Kwanza Wahida Mbaraka alisema kuwa wameandaa tamasha hilo kwa lengo la kuwakutanisha wateja wao na kupata burudani ya pamoja.

Mbaraka alisema kuwa maandalizi yake yamekamilika na wameandaa ulinzi mkali kwa ajili ya kuwalinda mashabiki katika tamasha hilo.

Alisema kuwa wapishi wa biriani zaidi ya 15 wa Dar es Salaam watakusanyika kwa pamoja katika tamasha hilo kwa ajili ya kutoa huduma hiyo ya chakula.

Alisema kuwa kampeni ya Biriani Friday na Coke imekuwepo kwa takribani miezi sita sasa ikiwa na malengo ya kuendeleza utamaduni wetu.

Alisema kuwa hakutakuwa na kiingilio kwa mashabiki wa burudani ambao wataingia kuanzia saa 4.00 asubuhi mpaka saa 11 jioni na na wale wataofika baada ya muda huo watalipia Sh3,000.