Saida Karoli kupamba 'Senene Festival' Kagera

Saida Karoli kupamba 'Senene Festival' Kagera

Muktasari:

  • Ni mara ya pili sasa tamasha hili linatarajiwa kufanyika Mkoani Kagera na kupambwa na burudani mbalimbali.

MUIMBAJI nguli wa nyimbo za kiasili Saida Karoli anatarajiwa kuwa miongoni mwa wasanii watakaopamba tamasha la 'Senene Festival' linalotarajiwa kutimua vumbi mwezi Disemba 24.

Mbali na Saida wasanii wengine 18 kutoka Mkoa wa Kagera wanatarajia kutoa wimbo maalumu katika kilele cha 'Senene Festival' kitakachofanyika Disemba 22 hadi 26 Mkoani humo.

Tamasha hilo la aina yake linatarajiwa kufanyika kwa mara ya pili kwa sasa baada ya mara ya kwanza kufanyika Februari 14 mwaka huu likiwa na lengo la kuwarejesha nyumbani wenye asili hiyo.

Akizungumza na waandishi wa habari mmoja wa wajumbe wa tamasha hilo msanii Anselm Tryphone 'Soggy Dogg' amesema kwa kutambua na kuheshimu asili yao na wingi wa wasanii wanaotoka Mkoa huo wako katika maandalizi ya wimbo ambao utazungumzia asili na mila zao.

Amesema Saida ni moja ya wasanii ambao amezitetendea haki nyimbo za asili akitokea Kagera hivyo atakuwa miongoni mwa watakaotoa burudani siku hiyo.

Amesema mbali na Saida pia watakuwepo Malaika, Bushoke, Lameck Ditto, Goodluck Gozbert na wengineo wakiwemo wasanii maarufu.

"Kwanza nilifurahia sana kuona wasanii wanaotoka Kigoma watani wetu hawa wakitunga wimbo wao inapendeza alafu wanatakiwa kujua wasanii wa Kagera tupo wengi sasa tutaenda kuwafunika watani zetu, "anasema Soggy.

Naye William Rutta amesma, wanahitaji kurejesha na kuwakumbusha wakazi wa Kagera ambao wako mjini kukumbuka na kuthamini tamaduni yao na hasa ikizingatia utalii umejaa Mkoani humo.

"Kutakuwa na vitu vingi kwenye hilo tamasha, Disemba 22-23 kutakuwa na semina kwa wajasiliamali, Disemba 24 elimu juu ya utunzaji mazingira, Disemba 26 ziara za kitalii katika maeneo ya kitalii pamoja na michezo ambapo kutakuwa na mbio fupi na pia kutakuwa na chakula pamoja na watu wenye uhitaji maalum, "anasema.

Huku Emmanuel Mwombeki anasema, tayari wameanza kupata sapoti kutoka kwa watu mbalimbali akiwemo Waziri wa Michezo na Sanaa Innocent Bashungwa na wengineo kwa ajili ya kufanikisha hilo.

"Nawaomba Wadau mbalimbali watusapoti ili kufanikisha tamasha hili ambalo tunatizamia kukifanya kuwa endelevu kuwakumbusha watu tamaduni zao, "anasisitiza.