Ray: Huyu Wema hapana,walisema nina miwaya

Muktasari:

Kutokana na ukimya wake, Ray hivi karibuni alikutana na Mwanaspoti na kufanya mahojiano ya kina akieleza mambo mbalimbali yanayohusu maisha yake.

MWIGIZAJI wa Bongo movie, Vincent Kigosi ‘Ray’ ni miongoni mwa mastaa wa Tanzania waliopata mafanikio kwenye tasnia hiyo, na kujijengea jina na heshima kwa jamii.

Kutokana na ukimya wake, Ray hivi karibuni alikutana na Mwanaspoti na kufanya mahojiano ya kina akieleza mambo mbalimbali yanayohusu maisha yake.

Mwananspoti: Mambo vipi Ray?

Ray: Poa tu, habari za siku nyingi?

Mwanaspoti: Nzuri tu, umepotea rafiki yangu, hata kwenye vyombo vya habari husikiki. Kulikoni?

Ray: Nipo tu, majukumu si unajua nina familia sasa hivi, na kuhusu kwenye vyombo vya habari sisikiki sababu napenda sana kusikika kwa ajili ya kazi zangu za filamu, sasa nilikuwa kwenye matayarisho ya filamu zangu hivyo mashabiki wakae mkao wa kula vitu vipya.

Mwanaspoti: Unalipi la kuwaambia mashabiki kuhusu utoaji wa filamu ulizozitayarisha, na utakuwa unatoa mfululizo au kwa awamu?

Ray: Kwanza kabla ya kutoa filamu zangu, ipo filamu nimeshirikishwa kutoka Zambia inaitwa ‘Imetosha’ hivyo mashabiki zangu waanzie hapo.

Mwanaspoti: Ni changamoto ipi ambayo hupata wasanii kukosa tuzo?

Ray: Unajua baadhi ya wasanii wengi wanashindwa kufahamu umuhimu wa kutopata tuzo pindi wanaposhirikishwa katika vipengele, yaani hakuna kitu kizuri kama kuwa na kipimo, sasa kukosa tuzo kwa msanii wa filamu ni changamoto, hivyo ukikosa inaongeza chachu ya kufanya kazi bora zaidi,na ndio hicho kipimo nachoongelea.

Mwanaspoti: Ukikutana na Waziri wa Habari, Utamadini, Sanaa na Michezo, Dk Harrison Mwakyembe unaweza kumwambia nini kuhusu filamu?

Ray: Kiukweli bila ya kupepesa macho na masikio, napenda Waziri siku moja apitie mikataba yote ya wasanii toka mwanzo wa kazi zao, huenda wasanii watafaidika na wasanii watarudishiwa sinema zao, maana tumefanya kazi kubwa, ila kwa sasa wanaofaidika ni wenye haki miliki, ndio maana sasa hivi tumejifunza kutokana na makosa, Kampuni ya MPTV ukipeleka kazi ndani ya mwaka mmoja wanakuachia inakuwa mali yako kwa hilo tunashukuru.”

Mwanaspoti: Unakipi cha kuzungumzia kwa Wema na Amber Ruth kuhusu video zao?

Ray: Naomba nilizungumzie hili suala kwa ufupi kidogo, kwanza hiyo video ya Amber Ruth sina shida naye atajua mwenyewe na maisha yake, nipo tayari kumzungumzia Wema sababu tumembrand sisi wenyewe.

Nakumbuka siku moja pale Lamada Hotel, Marehemu Kanumba kipindi wanaanza mahusiano na Wema alinifuata na kuniuliza kuwa anafaa kuigiza Wema? Maana kulikuwa kunatakiwa waigizaji wapya wa kike wacheze filamu ya ‘A point of no Return’ basi tukaanzia hapo. nikaona anaweza na Wema ndio ilikuwa filamu yake ya kwanza,na ndio maana nasema ananihusu

Sasa kwa upande wa kumzungumziaje kuhusu hizo video, Wema amekosea sana na sio mara ya kwanza kukosea, chamsingi ajijue yeye ni brand na sasa hivi hakuna kampuni itakayoweza kufanya kazi na Wema kutokana na tabia zake alizozionyesha.

Hivyo ajirekebishe na sio awaaminishe Watanzania kuwa amebadilika ili aweze kufanya kazi nao ajaribu kuwaaminisha Watanzania kuwa amerekebishika sababu ukiangalia hakuna mtu asiyefanya mapenzi, hata mimi nafanya mapenzi na sio katika mitandao.

“Mtu gani anaomba msamaha kila siku mambo yaleyale, Watanzania wanampenda ila asiwaangushe, kiukweli adhabu aliyopewa anastahili kabisa Wema.”

Na niseme tu asilimia ya Watanzania wanapenda kuambiana vitu vya kusifiana na sio kukosoana sitaki kukumbatia maneno, sijapendezwa na niseme tu sitaki na sitamani kumshirikisha kwenye kazi zangu,maana najua ataichafua na kuchafua tasnia ya filamu, yaani hajui kama anaharibu jina lake, na kwani hupati jina hadi skendo?, mimi nilikuwa na skendo za kibinadamu na sio kama Wema na sasa sizitaki hizo skendo”

Mwanaspoti: Ulijisikiaje siku ya kwanza kusikia chuchu ana ujauzito wako?

Ray: Nilijua ni mchezo tu, maana mara nyingi alikuwa akipata ujauzito inaharibika, hata alivyokuja kuniambia anaujauzito nikajua niyale yale tu lakini siku zilivyozidi kwenda nikajua sasa ni kweli na nikasema Mungu ni mwema, maana nilikuwa ndio kilio cha muda mrefu, na furaha ilizidi kupata mtoto wa jinsi kiume japo mama yake alikuwa anataka wa kike.

“Chuchu alivyokuwa mjauzito, mambo mengi yalikuwa yanaongelewa, mara oooh Ray mgonjwa wa Ukimwi, mara sina kizazi, sasa Mungu amewauumbua wambea na wanafki.

Mwanaspoti: Una kipi cha kuhusu, Irene Uwoya kudaiwa kuvunjika kwa ndoa yake?

Ray: Kuhusu ndoa ya Irene Uwoya kwakweli siwezi zungumzia hilo maana sijui kitu,na siwezi mshauri masuala hayo, ila nampenda Irene kwa sababu yuko makini kutafuta pesa na mshauri afanye kazi vitu vingine ni ziada.

Mwanaspoti: Mashabiki zako wategemee lini ndoa yako na Chuchu Hans?

Ray: Mimi nitaoa tu muda ukifika nitaweka wazi, sababu nipo kwenye uhusiano na Chuchu niliweka wazi na hata ndoa nitaweka wazi bila ya kuficha.

Mwanaspoti: Shukrani sana.

Ray: Haina noma.