Prime
Mobetto afichua siri mwaka mmoja ndoa na Aziz Ki
NI mwaka mmoja na mwezi mmoja umepita tangu Stephane Aziz KI afunge ndoa na Hamisa Mobetto ambapo mwenyewe amesema ndani ya kipindi hicho, kuna mambo mengi yamebadilika katika maisha yake ikiwemo muonekano uliotokana na amani ya moyo aliyonayo kwa sasa.
Ndoa hiyo ilifungwa Februari 16, 2025 jijini Dar es Salaam huku ikihudhuriwa na watu mbalimbali maarufu.
Akizungumza na Mwanaspoti, Hamisa ambaye ni mfanyabiashara na mwanamitindo huku pia akijihusiha na sanaa ya uigizaji na uimbaji, amesema kila siku wanayoishi pamoja mume wake Aziz KI, ni historia mpya wanayoijenga na kila changamoto wanayoshinda pamoja huwa wanasherehekea wakiwa ndani.
“Kwa sisi, mpya si tu siku mpya, bali ni kila tukio linalojenga uhusiano wetu, hivyo kila changamoto tunapoishinda, tunasherehekea ushindi wetu pamoja tukiwa wawili tu ndani ya nyumba,” amesema Hamisa.
Hamisa alifafanua kuwa, ndoa yao imejengwa kupitia vitendo na si maneno tu, mshikamano wao huonekana kila siku, na huo ndio msingi wa furaha na mshikamano wa kweli.
“Mapenzi yetu yamejengwa kwa vitendo na namna unavyomjali mwenza wako, unavyomwelewa na kusamehe hata pale mambo yanapokuwa magumu,” amesema.
Aidha, Hamisa alifafanua mabadiliko aliyoyapata tangu kuolewa akisema amepata amani ya kweli na hivi sasa mvuto umeongezeka.
“Nimekuwa na amani ya kweli, nimefurahia maisha ya ndoa, nimepata furaha na utulivu hadi mwili wangu umebadilika kidogo, nimeongeza furaha na mvuto wangu umeongezeka kwa sababu ya maisha tuliyonayo sasa na mume wangu Aziz Ki,” amesema Hamisa.
Mrembo huyo pia alielezea jinsi anavyomhudumia mumewe kila siku, akithamini kila kitu kizuri anachopika. “Ni furaha kubwa kuona mume wangu akipenda kile ninachomtayarishia na kufurahia kila muda unaotumika kumhudumia, hii ni moja ya njia tunayojenga mshikamano wetu kila siku,” amesema.
Hamisa alisisitiza kuwa ndoa inahitaji uvumilivu na usikivu wa kila mmoja.
“Wengi walidhani haitadumu, wengine wamesema hata mwaka sifikishi, lakini leo tumefikisha zaidi ya mwaka mmoja, ndoa si kitu cha kuchezea, ni kuchagua kumpenda mwenza wako kila siku,” amesema.
Kwa sasa, Hamisa anasema hawaangalii kelele za watu waliokuwa wakihofu juu ya ndoa yao, badala yake anataka kuendelea kujenga maisha yao kwa upendo, mshikamano, uvumilivu na furaha ya kila siku.
Wakati Aziz KI raia wa Burkina Faso anamuoa Hamisa Mobetto, alikuwa akiichezea Yanga, kisha akaenda Wydad AC ya Morocco na sasa anaitumikia Al-Ittihad ya Libya.