Majizo ataja sababu ya kufunga ndoa kimyakimya na Lulu

Muktasari:

  • Majizo na Lulu walifunga ndoa ya kimyakimya Februari 16, mwaka huu baada ya kuvalishana pete ya uchumba miaka miwili iliyopita.

Mfanyabiashara na mmiliki wa kituo cha redio Efm na TvE, Francis Ciza marufu ‘Majjizo’, ameeleza sababu ya kufunga ndoa ya kimyakimya na msanii wa filamu nchini, Elizabeth Michael ‘Lulu’.

Majizo amesema hayo leo Jumatatu Aprili 19, 2021 alipohojiwa katika kipindi cha Joto la asubuhi cha Efm.

Majizo na Lulu walifunga ndoa Februari 16, mwaka huu  katika kanisa la  St Gasper lililopo Mbezi  Beach, Dar es Salaam na kuhudhuriwa na watu wachache.

Katika mahojiano hayo swali aliloulizwa Majizo na mtangazaji ni kwa nini alifunga kufunga ndoa ya namna ile na msanii Lulu.

Akijibu amesema: "La kwanza nilitaka kuwaonyesha vijana unaweza kufunga ndoa hata kama una kitu kidogo.

“Ningeweza kuwa na watu zaidi ya 3,000 lakini nilitaka nisiwatishe...harusi haikuwa ya gharama ukiachilia mavazi,” amsema Majizo na kuongeza:

 “Lakini pia nilitaka kufanya jambo la kiroho tu na wazazi walitupa 'support' kubwa. Mimi nina marafiki wengi ningetaka kuchangisha wangejaa na Elizabeth naye ana marafiki wengi Bongo movie yote wangejaa.”

Hata hivyo, mfanyabiashara huyo amesema cha msingi anachowasisitiza vijana ni kutoogope kufunga ndoa, kwani si lazima ufanye kitu kikubwa.