Magufuli akunwa na ‘Baba’ ya Stamina ft Profesa Jay

Muktasari:

  • Rais wa Tanzania John Magufuli amezindua jingo la Jitegemee lenye studio mpya za Channel 10 na Magic Fm jijini Dar es Salaam, huku akiomba kupigiwa wimbo wa Profesa Jay na Stamina ‘Baba’.

Dar es Salaam. Rais wa Tanzania John Magufuli ameomba kupigiwa wimbo mpya wa Stamina aliowashirikisha Professor Jay na One Six unaoitwa Baba alipokuwa anazindua studio za Channel 10 na Magic Fm.

Magufuli ameomba kupigiwa wimbo huo akiwa ndani ya studio hizo leo Februari 25, 2020 ikiwa ni siku ya pili ya ziara yake ya siku tatu aliyoipanga kuifanya jijini humo.

Mara baada ya kukata utepe wa kuzindua rasmi studio hiyo alianza kupita katika vyumba mbalimbali vya studio hiyo na baadaye akiingia katika chumba cha kutangazia habari cha Channel 10 televisheni na kuzindua kwa kubonyeza kitufe kisha akasema;

“Nipigieni ule wimbo wa Profesa Jay ambao alikuwa anaongea na baba yake, Naongea na Wewe,” alisema Rais Magufuli mara baada ya kuzindua rasmi studio hizo.

Wakati akisikiliza na kuangalia video hiyo kupitia luninga iliyopo ndani ya studio hizo alionekana kupendezwa na nyakati zingine alikuwa akiimba kwa sauti ya chini huku akitingisha kichwa, alisikiliza wimbo huo kwa zaidi ya dakika mbili.

Baada ya kumaliza kuusikiliza amesema, “Huu wimbo una meseji, lakini hongereni sana.”