Lulu Diva atoa onyo kuhusu Wema Sepetu
Muktasari:
- Lulu Diva ambaye ni rafiki mkubwa na msanii huyo wa Bongo Movie, ameliambia Mwanaspoti anakerwa sana na kuumizwa kuona rafiki yake, ambaye anatamani mtoto kwa muda mrefu, akiwa anajibu maswali kwa kusononeka hadi kufikia hatua ya kukata tamaa ya kupata mtoto.
MSANII wa Bongo Flava, Lulu Diva anayetamba na nyimbo kama Utamu, Ona, Amezoea, Nilegeze na nyingine, amesema ifikie mahala watu waache kumuuliza Wema Sepetu kuhusu kupata mtoto.
Lulu Diva ambaye ni rafiki mkubwa na msanii huyo wa Bongo Movie, ameliambia Mwanaspoti anakerwa sana na kuumizwa kuona rafiki yake, ambaye anatamani mtoto kwa muda mrefu, akiwa anajibu maswali kwa kusononeka hadi kufikia hatua ya kukata tamaa ya kupata mtoto.
"Mimi ingekuwa amri yangu, watu ama media zingeacha kumuuliza Wema habari za kupata mtoto, maana hili jambo ameshaliongea sana huko nyuma hadi kufikia hatua ya kukata tamaa nalo, sasa anapoulizwa kila wakati inakuwa kama kumkufuru Mungu tu, halafu mie kama mtu wake wa karibu huwa naumia sana japo najua kuna watu wengine pia wapo wanaumia sababu ya wema kwenye suala hili."
"Mfano tuangalie tu kipindi hiki anachopitia Wema kuhusu kutaka mtoto muda mrefu na bado hajafanikiwa, ndiyo kiwe kwako unadhani utajisikiaje? Niwaambie tu Wema huwa anajibu tu kwa ujasiri lakini baada ya hapo huwa anakosa raha sana, yaani inakuwa kama anatonyeshwa kidonda upya, kikubwa ni kumwombea kwa Mungu ajaaliwe kwani tumeona wapo watu waliokata tamaa ya uzazi lakini wakaja kupata watoto," alisema Lulu Diva.
Hivi karibu Wema Sepetu alionekana Dodoma kwenye uchaguzi mkuu, akafanya mahojiano na baadhi ya media akasikika akisema kuwa amekata tamaa ya kupata mtoto na kilichobakia sasa hivi atalea watoto wa ndugu zake au marafiki zake.
Mbali na hayo, Lulu Diva alisema ni upuuzi kwa msanii kutomheshimu shabiki wake kwa kuwa bila huyo hawezi kuwa msanii.
Lulu Diva alisema kwa kuwa msanii ni kioo cha jamii, hivyo hatakiwi kutoheshimu mashabiki wake kwa kuwa hao ndiyo wanaomsaidia kisanii.
“Kuna baadhi ya wasanii wanatumia majina yao vibaya, ukiwa staa unatakiwa uwe ‘smart’ ujipende, uwe na upendo na wenzako, uwe mvumilivu unayejiheshimu na kuheshimu watu wako wakiwamo mashabiki," alieleza Luu Diva