Linex afichua ishu yake na Baba Levo
MSANII wa Bongo Fleva, Sunday Mangu 'Linex Sunday Mjeda' amesema alichokizungumza Mbunge wa Kigoma Mjini, Clayton Revocatus Chipando 'Baba Levo' anatambua fika harakati za upambanaji wa vijana mtaani.
Miongoni mwa hoja alizozitoa Baba Levo bungeni ni masharti ya mikopo kwa vijana ambapo alimtolea mfano Linex kwamba wakimuhitaji apeleke hati ya nyumba atatoa nini wakati hana, jambo ambalo limepokelewa vizuri kwa staa huyo.
"Baba Levo kabla hajawa mbunge anaelewa hali halisi za vijana mtaani, hivyo akiongea kitu ujue kiliwahi kumgusa maisha yake, ndiyo maana anatamani wengine wapige hatua," amesema Linex na kuongeza;
"Katika haso zake nilikuwepo na katika haso zangu alikuwepo, hawezi kuacha kuniongelea mimi ama siwezi kuacha kumuongelea yeye kwa namna moja ama nyingine. Mfano alioutoa unabeba vijana wengi nyuma yake.
"Niliwahi kufanya mahojiano na wewe (mwandishi) kuhusu Baba Levo wakati akifanya kampeni za ubunge, nilikwambia mbali na ucheshi wake ni mpambanaji na jasiri kuongelea kitu anachokiamini, nadhani sasa unajiona anachokitamani kifanyike kwa vijana wenzake."
Amesema kwa miaka ya sasa kijana akifikisha umri wa miaka 30 hapaswi kuendekeza 'ubrazamen' kwa msichana 'usistaduu' hivyo haviwasaidii kama hajaweza kuweka misingi yake ya kiuchumi anakuwa anaiendea njia ya umaskini.
"Ndiyo maana kwa sasa kijana akiwa chuo anasoma tayari anakuwa amefahamu njia za kumuingizia pesa, tofauti na miaka ya nyuma, vijana wanahitaji pesa siyo maneno," amesema Linex anayetamba na wimbo wa Furaha aliyomshirikisha Dully Skykes.