Kusah ameamua kupita njia yake kisanaa
Muktasari:
- John ambaye ni mshindi wa 19 wa tuzo za EGOT katika historia, amechangisha zaidi ya Dola 125 milioni kwa ajili ya shirika lake la kupambana na Ukimwi.
WAKATI Waingereza wana Elton John, Tanzania yupo Salmin Ismail Hoza maarufu kama Kusah. Hawa wote ni wasanii na watunzi wa muziki ambao kila mmoja amekuwa akiigusa jamii kwa namna yake.
John ambaye ni mshindi wa 19 wa tuzo za EGOT katika historia, amechangisha zaidi ya Dola 125 milioni kwa ajili ya shirika lake la kupambana na Ukimwi.
Ukirudi Tanzania ukiacha marafiki kufurahishwa na moyo wa Kusah wa kujitoa, staa wa Bongofleva Ali Kiba aliwahi ‘kukomenti’ katika mtandao wa kijamii wa Instagram akifurahishwa na Kusah kugusa watu wengine.
Miezi saba iliyopita akiwa nyumbani kwao Bumbuli, Tanga alionekana akimkabidhi kiti cha magurudumu (wheel chair), redio na nguo rafiki yake aliyetajwa Ally mwenye ulemavu wa miguu.
Kusah alilizungumzia hilo akisema: “Ally ni rafiki yangu natamani kabla sijaiaga dunia nimuone tukae tumsomeshe hadi chuo. Kwa sasa acha nimjengee, nimfungulie biashara kisha apate mke ipo siku nitawaalika katika harusi yake. Mwenyenzi Mungu anajua.
Aliongeza: “Ali Kiba niliona komenti yake kufurahishwa na kile nilichokifanya kwa Ally. Naheshimu na namshukuru.”
Mbali na Ally kuna mwimbaji mwenye ulemavu wa macho anayejulikana kwa jina la Godfrey Mteule aliyekuwa anaimba mitandaoni aliyempa sapoti ya kurekodi naye kolabo ya wimbo wa ‘Huyu Mungu ni wa Ajabu’.
Kusah aligusa katika sekta ya michezo kwa kutoa jezi kwa timu ya soka ya walemavu ya Sauti Paraspoti na katika video alionekana akifurahia nao na akapata muda wa kuwaimbia nyimbo zake mbalimbali. Kuna video nyingine aliiposti katika mtandao wa Instagram ilimuonyesha akimpatia kiasi cha Sh50,000 aliyemtaja kwa jina la Festo (umri wa miaka 25) aliyekuwa anafanya kazi ya kuokota makopo mitaani.
Kusah alionekana kuondoka na kijana huyo hadi nyumbani kwake, na mbali na kula naye chakula alimpatia zawadi mbalimbali, akambadilishia nguo na kumpa mpya, akamvalisha raba kisha akaondoka na usafiri wa bodaboda.
Kusah akiwa na mama watoto wake, Aunty Azekiel aliyezaa naye watoto wawili (Nono na Zara) walionekana kupika chakula kisha wakaenda kukigawa mtaani.
Kusah aliwahi kuandika katika mtandao wa Instagram kwamba anachokifanya ni mradi anaoamini huko mbeleni atafanya makubwa zaidi na itakumbukwa vizazi na vizazi.
Kabla ya kupata umaarufu mkubwa katika tasnia ya muziki nchini, Kusah alikuwa mwandishi wa nyimbo akiwaandikia wasanii wakubwa kama Ali Kiba, Nandy, Ben Pol, Ruby na wengineo wengi.
Kusah alianza kujulikana sana baada ya kutoa wimbo wake wa Kelele akimshirikisha Ruby 2018. Tangu wakati huo ameshatoa nyimbo nyingi zilizofanikiwa kama I Don’t Care, Nibebe, Mama Lao na I Wish ambazo zimekusanya zaidi ya ‘streams’ milioni 10 kwenye Boomplay.
Septemba 2022, Kusah alitoa EP ya kwanza itwayo Romantic EP akiwashirikisha Johnny Drille kutoka Nigeria na Femi One wa Kenya. EP hiyo ilipokewa vizuri.Ndani ya mwaka huo pia aliteuliwa kwenye Tuzo za Muziki Tanzania kama Msanii Chipukizi Bora.