Kumbe Bright kabla ya kuachia nyimbo anafanya utafiti...

MSANII wa kizazi kipya anayejulikana kwa jina la  Rashid Said 'Bright' amesema kabla ya kuandika wimbo na kuachia, anazingatia mahitaji yaliyopo kwenye jamii husika.

Bright amesema kutokana na vipaji vya wasanii kuibuka kila kunapoitwa leo na ushindani kuwa mkubwa sokoni, jambo la msingi kwake ni kufanya muziki unaowagusa walaji wa kazi zake.
 
"Muziki unahitaji akili na kufanya utafiti mkubwa wa kujua unaowapelekea wanahitaji nini, hivyo vitu  ni muhimu zaidi kuliko kufanya ushindani usio na tija," amesema Bright na ameongeza;

"Ndio maana kila msanii anatambulika kwa aina yake ya uimbaji na utunzi anakuwa ameyafanyia kazi anayoyaimba," amesema.

Ametolea mfano wa kibao chake cha Nitunzie alichomshirikisha Baraka the Prince, ndani yake kimebeba ujumbe wa mapenzi namna yanavyowaumiza wengi.
"Mapenzi ni matamu upopata mnayependana, vilevile ni machungu unapopenda pasipopendeka ni ujumbe ambao unamhusu kila mtu kwa namna yake," amesema.

Baadhi ya nyimbo nyingine alizowahi kutamba nazo Bright ni Umebadilika aliomshirikisha Nandy, Mazonge kaimba na Jolie, Nakuja Dar kamshirikisha Stamina na Morogoro.